TOHARANI NI WAPI NA INAPATIKANA WAPI KWENYE BIBLIA?

 



 

TOHARANI NI WAPI NA INAPATIKANA WAPI KWENYE BIBLIA?

(Naomba ni kushirikishe kusoma habari hii nzuri juu ya Toharani ambayo nimeikuta mahali bila kupunguza au kuongeza neno naomba Tusome pamoja tujifunze kitu.

 

• Iko hivi...

 

Kwa mujibu wa Katekisimu ya Kanisa Katoliki, Toharani inaelezwa kama Utakaso wa mwisho (final purification). Yaani wale wote waliokufa katika Huruma ya Mungu, na urafiki na Mungu. Lakini hawakuwa Safi kabisa, lazima waende kwanza Toharani ili wakatakaswe kabla ya kuingia Mbinguni.

 

Ile hali ya Utakaso kabla ya kuingia Mbinguni, ndio tunaiita "Toharani" na fundisho hili linaadhimishwa rasmi ndani ya Kanisa kupitia Mitaguso ya Florence na Trent. (Rejea Catechism Of The Catholic Church 1030-31).

 

Kamusi ya Concise Oxford inaeleza neno "Toharani"  kama eneo, sehemu au hali ya mateso inayopata roho za wenye dhambi ndogo kama malipizi yake, ili itakasike kabla ya kuingia Mbinguni.

 

"A place or state of suffering inhabited by the souls of sinners who are expiating their sins before going to Heaven".

 

Kwa Kingereza Toharani hujulikana kama "Purgatory", kwa Kilatini ni "Purgatorium".

 

Maneno yote haya yana maana moja kuwa, ni eneo la Utakaso kwa roho zenye dhambi nyepesi kabla hazijaingia Mbinguni.

 

Neno "Toharani" au "Purgatory" halipo kwenye Biblia, iwe ya tafsiri ya Kiswahili au English version n.k

 

Hali kadhalika hata neno lenyewe "Biblia" halipo kwenye Maandiko Matakatifu, yaani Biblia yenyewe haijataja kama inaitwa "Biblia".

 

Vile vile neno "Utatu" au "Trinity" hauwezi kulipata sehemu yoyote ile kwenye Biblia, lakini haimaanishi kwamba hakuna fundisho linalotupa tusiamini uwepo wa Utatu Mtakatifu.

 

Kwahiyo neno kutotajwa kwenye Biblia, haifanyi neno hilo lisiwepo. Kwani pale Biblia haijapataja, basi Mapokeo yana kitu cha kutuambia.

 

Hakika Biblia ilibuniwa ili kuyataja yale Maandiko Matakatifu yaliyojumuishwa pamoja. Vivyo hivyo neno "Toharani" limebuniwa ili kuwakilisha eneo au hali ambayo zile roho zilizotenda dhambi nyepesi zinapelekwa pale ili kutakaswa kabla ya kuingia Mbinguni.

 

Fundisho kuhusu Toharani limetajwa kwenye Biblia katika Kitabu cha pili cha Wamakabayo na Injili ya Mathayo. 

 

Kumbuka, neno "Toharani" halipo ila "Concept" kuhusu Toharani ipo.

 

Ukatoliki haujajengwa tu kwa Maandiko Matakatifu (Sola Scriptura), bali pia katika Mapokeo Matakatifu.

 

Kwani kupitia Maandiko na Mapokeo Matakatifu, ndipo misingi ya mafundisho ya Kanisa Katoliki yanapatikana.

 

*CONCEPT AU FUNDISHO KUHUSU TOHARANI TUNAIPATA WAPI KWENYE BIBLIA?*

 

Nini tunakipata katika Kitabu cha pili cha Yuda Makabayo, moja ya vitabu vinavyopatikana tu kwenye orodha ya vitabu vya Biblia Takatifu.

 

Deuterocanonical books ambapo Waprotestanti wanakiweka kwenye orodha ya vitabu vya "Apocrypha" yaani "Vitabu visivyokubalika".

 

Basi naomba rejea 2Makabayo 12:39-45 inasema:

 

39. Siku iliyofuata waliona ni haraka na muhimu kukusanya miili ya wenzao waliokuwa wameuawa vitani, na kuizika katika makaburi ya wazee wao.

 

40. Lakini katika kila maiti, walikuta zimefichwa nguo sanamu ndogo ndogo za miungu iliyoabudiwa yamnia, jambo ambalo sheria inawakataza Wayahudi kuzivaa. Hapo kila mtu alijua ni kwanini hao walikuwa wameuawa.

 

41. Hivyo wakazisifu njia za Bwana Hakimu mwenye Haki, afichuaye vilivyofichika.

 

42. Na wakamwomba Bwana afutulie mbali dhambi hiyo, kisha Yuda yule mtu mwadilifu akawataka watu waepuke dhambi, kwa sababu walikuwa wamejionea wenyewe yaliyokuwa yamewapata wale waliokuwa wametenda dhambi.

 

43. Pia alichangisha fedha kutoka kwa watu wake, fedha ipatayo drakma elfu mbili akaipeleka Yerusalem kwa ajili ya dhabihu ya kuondoa dhambi. Yuda alifanya tendo lililo jema, kwa sababu aliamini katika ufufuo wa wafu.

 

44. Kama asingekuwa na imani kwamba wafu watafufuliwa, ingekuwa ni upambavu na kazi bure kuwaombea marehemu.

 

45. Lakini akiwa anatazamia tunzo nzuri walioekewa waliokufa wakiwa waaminifu kwa Mungu, hilo lilikuwa wazo jema na takatifu. Kwahiyo Yuda alitolea dhabihu ya upatanisho, ili wote wapate kuondolewa dhambi zao.

 

Myahudi Yuda Makabayo alifanikiwa kuongoza vita dhidi ya Mfalme Antrochus IV wa Syria, kati ya mwaka 167 - 160 BC.

 

Baadhi ya maaskari wake walifia vitani, katika kupekua maiti zao ndipo Yuda na wenzake wakagundua kuwa, baadhi ya wale maaskari waliokufa walikuwa wamevaa visanamu vya bahati viunoni na shingoni, tuseme ni kama yale makonokono ya baharini, ambazo baadhi yetu tunawavalisha watoto wetu, eti kuwakinga na watu wenye macho mabaya.

 

Sasa Hawa Askari walivaa visanamu vya miungu yamnia kama kinga yao wasiuawe vitani.

 

Katika sheria ya Torati ya Musa na Amri za Mungu, hii ilikuwa ni kosa kubwa mno kwa Wayahudi kwa kuwa Amri ya kwanza ya Mungu iliwakataza kufanya hivyo.

 

Kiufupi askari hawa walikuwa wametenda dhambi, japo walikuwa katika mapambano ya kutetea imani yao, watu watu na taifa lao la Israel kwa ujumla.

 

Kwahiyo baada ya Yuda kuona hivyo, hakuwaacha bali alifanya sala ya toba kwa ajili yao, na hata kutoa dhabihu ya maondoleo ya dhambi zao. Kitu alichokifanya Yuda, ndicho kinachofanywa na Wakatoliki hadi leo.

 

Hebu pia angalia Mathayo 12:32, inasema:

32. Tena asemaye neno la kumpinga Mwana atasamehewa, lakini yule asemaye neno la kumpinga Roho Mtakatifu hatasamehewa katika ulimwengu huu wala ule ujao.

 

Hapa Yesu anasema nini? Kwamba dhambi zote zitasamehewa, ila ile ya kumkufuru Roho Mtakatifu haitasamehewa kwenye ulimwengu huu (duniani) wala ule ujao (toharani).

 

Kwa tafakari ya kina Yesu anatuambia kwamba, kuna maondoleo ya dhambi sehemu mbili, katika ulimwengu huu na ule ujao.

 

Huo ulimwengu ujao ambao kuna maondoleo ya dhambi ni upi? Biblia haijatupa jina, lakini kupitia Mapokeo Matakatifu ya Kikatoliki sisi tumeuita ni "Toharani".

 

Kumbe basi kama dhambi zako hazikuondolewa katika ulimwengu huu wakati ulipofariki, kuna uwezekano zikaondolewa katika ulimwengu ujao. Ikiwa itafanyika Ibada ya maombezi kama ile aliyoifanya Yuda Makabayo, kwa wale maaskari wake waliofia vitani.

 

Ikumbukwe, Yesu anasema sio kila dhambi itaondolewa kwenye ulimwengu ujao (Toharani), kama dhambi ya kumkufuru Roho Mtakatifu.

 

Mtu kama yupo motoni (hell) hakuna sala itakayomfikia, kwani kuna ukuta mkubwa sana kati yetu na wao. (Luka 16:25-26).

 

Lakini kama mtu huyo yuko Mbinguni (Heaven) hakuna sala inayohitajika juu yake. Lakini kama sasa ikitokea mtu huyu hastahili kwenda motoni wala kuingia Mbinguni, moja kwa moja kuna sehemu atakwenda kwanza, sehemu hiyo anaweza kuombewa kama Yuda Makabayo alivyofanya.

 

Sasa kwanini sehemu hiyo tusiipe jina? Kama ilivyo Mbinguni na motoni, sehemu hii nayo inastahili kupewa jina la utambulisho.

 

Kanisa Katoliki limepaita mahali hapo kuwa ni Toharani. Jina hili halipatikani mahali popote, lakini Mapokeo Matakatifu yanatuambia panaitwa Toharani.

 

Mapokeo Matakatifu yanatuambia kuwa, Toharani sio sehemu ya kungojea hukumu au sehemu ya kifungo, bali ni mahali pa Utakaso kabla ya kuingia Mbinguni.

 

Mafundisho ya Kanisa Katoliki yanasema kuwa, Toharani sio chumba cha mateso, bali ni kama chumba cha maandalizi kabla ya kuingia Ikulu ya Mfalme Yesu Kristo.

 

Dhambi kubwa hukumu yake ni kwenda jehanamu, ila dhambi nyepesi ambazo hazikutendwa kwa makusudi, utakaswa Toharani.

 

Amini kwamba, Toharani ipo na ni fundisho halali la Kikatoliki linaloonesha kukubalika bila mashaka yoyote (dogma), lakini fundisho kuwa kila roho lazima ipite Toharani kabla ya kwenda Mbinguni hilo sio fundisho la Kanisa Katoliki.

 

Fundisho la Toharani lilipewa mkazo zaidi na Papa Gregory Mkuu (590 - 604 AD) Kanisa Katoliki lilifafanua fundisho hili na kuliweka rasmi katika Baraza la Lyons (1274), na Baraza la Florence (1439) na lilakazaniwa zaidi kwenye Baraza la Trent (1547). Kumbuka Baraza ndio Mtaguso kwa jina lingine.

 

Paulo aliwauliza Wakorintho (1Kor 15:29) kuwa:

29. Kama hakuna ufufuo, je watu wale wanaobatizwa kwa ajili ya wafu wanatumaini kupata nini? Kama wafu hawafufuliwi, ya nini kubatizwa kwa ajili yao?

 

Kumbe mtazamo wa Mtume Paulo na Yuda Makabayo juu ya kuwaombea wafu, walikuwa sahihi kwa watu wote waliotumaini juu ya ufufuo wa wafu.

 

Paulo anaendelea kusema (1Kor 3:13-15) kuwa:

13. Iwe iwavyo ubora wa kazi ya kila mtu mmoja utaonekana wakati siku ile ya Kristo itakapoifuchua. Maana siku hiyo itatokea moto, na huo moto hutapima na kuonesha ubora wake.

14. Ikiwa alichojenga mtu juu ya huo msingi, kitastahimili huo moto, atapokea tuzo.

15. Lakini kama alichojengwa kitaunguzwa, basi atapoteza tuzo lake. Lakini yeye mwenyewe ataokolewa, kana kwamba ameponyoka kutoka motoni.

 

Rejea ule mstari wa 15 unaosema: "Inaweza ikawa ulichojenga kikaunguzwa, yaani haukustahili kupewa tuzo, lakini bado ukaolewa kwa mithili ya kuponyoka.

 

Hii ina maana kuwa, sio wote watakaonekana kuwa wenye dhambi, basi wataenda motoni, wako ambao watakaonekana. Kwa tafakari ya kina, hao watakaoponyoka ni wale ambao roho zao ziko Toharani.

 

Aya hii ya 15 unaweza ukaielewa zaidi kama utaisoma tena kwa tafsiri ya Kingereza:

 

"If anyone's work is burned up, he will suffer loss, though he himself will be saved, but only as through fire" (1Cor 3:15).

 

Kwa maelezo haya machache, naamini utakuwa umenielewa.

 

 

*RAHA YA MILELE UWAPE EE BWANA...*

 


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

JINSI YA KUSALI ROSARI TAKATIFU YA BIKRA MARIA

ROZARI YA KUWAOMBEA MAREHEMU TOHARANI

MALAIKA MKUU MT. MICHAEL UTULINDE KATIKA VITA

IBADA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

TAMBUA UMUHIMU WA KUOMBEA MIMBA KWA MAMA MJAMZITO

CHANGAMOTO YA NDOTO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO