HISTORIA YA MAISHA YA BIKIRA MARIA


 

HISTORIA YA MAISHA YA BIKIRA MARIA

MAISHA YA WAZAZI WA BIKIRA MARIA

Mnamo karne ya pili kabla ya kuzaliwa kwake Bwana wetu Yesu kristo. Wazazi wa Bikira Maria walijulikana katika Kanisa kwa majina ya JOAKIMU na ANNA. Hata ilipofika karne ya nne, Wakristu wa kanisa la Mashariki walikuwa tayari wameshazoea kuwaheshimu wazazi hawa. Mwaka 1548 Kanisa Katoliki lilianza rasmi kusherekea sikukuu ya wazazi wa Mungu, Katika kalenda ya Kanisa sikukuu ya Watakatifu hawa huadhimishwa tarehe 26 Julai kila mwaka.

BABA MZAZI WA BIKIRA MARIA

Joakimu ndiye Baba mzazi wa Bikira Maria, Baba huyu alikuwa wa kabila la Yuda na Ukoo wa Mfalme Daudi. Jina Joakimu lina maana ya Matayarisho kwa ajili ya Bwana ; au Bwana anatayarisha. Mtakatifu huyu aliishi Nazareti iliyoko Galilaya.

MAMA MZAZI WA BIKIRA MARIA

Anna ndiye mzazi wa Bikira Maria, Mama huyu alizaliwa katika ukoo wa Haruni Kuhani Mkuu wa kabila la Yuda. Jina la Anna lina maana ya Neema au Enye Neema. Mama huyu nyumbani kwao kulikuwa Betheremu mji wa Yerusalemu. Huko ndiko alikoishi kabla ya kuolewa.

JOAKIMU NA ANNA WACHA MUNGU HATA KABLA YA NDOA

Kutokana na maasi ya wanadamu kwa Mungu wao, Nyakati hizo, kabla ya Joakimu na Anna kufunga ndoa, Watu walikuwa wamechanganyikana katika makundi mawili, kwanza kulikuwa na kundi la watu wacha Mungu na kundi la pili la watu wasiomcha Mungu.

Lakini Joakimu alikuwa mcha Mungu sana na siku zote alisali akimuomba Mungu mambo mawili, nayo ni mosi Masiha azaliwe ili aikomboe Dunia katika Maasi, pili aliomba apate mke mwema na mcha Mungu kama yeye mwenyewe, Pia Anna alikuwa msichana mcha Mungu sana, naye alisali kila siku akimuomba Mungu mambo mawili vivyo hivyo kama Joakimu. Masiha aje mapema na apate Mume mcha Mungu kama yeye mwenyewe. Ili waendeleze sala zao kwa pamoja wakiomba Mungu Masiha aje haraka na kuikomboa dunia katika uasi na dhambi.

Wakati Joakimu na Anna walipokuwa wakiomba hayo walikuwa hawafahamiani kabisa, wala hawakujua kama siku moja watakuwa Mume na Mke. Kwani kila mmoja wao alikuwa akisali nyumbani kwake. Joakimu akiwa Nazareti na Anna akiwa Betheremu. Lakini kitu cha kushangaza na cha ajabu ni kwamba, kwanza sala zao na nia za maombi yao zilifanana. Halafu saa au muda aliokuwa akisali kule kwake Nazareti hata Anna naye alikuwa akisali kule kwao Betheremu.

MALAIKA GABRIEL ANAWAPASHA HABARI ZA UCHUMBA.

Siku zilipita nyingi Watakatifu hawa walidumu katika sala na kumtukuza Mungu. Na kila waliposali hawakuacha kumweleza Mungu maombi yao hayo mawili, yaani Masiha aje haraka na kila mmoja wao apate mchumba ambaye ni mcha Mungu. Basi mwisho Mungu akasikiliza sala na maombi yao; kama yasemavyo maandiko Matakatifu, Ombeni mtapewa, tafuteni mtapata, pigeni hodi mtafunguliwa. Math 7:7-11 ndivyo Mungu alivyofanya kwa Joakimu na Anna. Siku moja Mungu alimtuma malaika Gabriel awapelekee ujumbe wa furaha kwa kila mmoja wao kwamba watakuwa watu wa ndoa. (Mume na Mke).

Anna alikuwa wa kwanza kutokewa na malaika Gabriel na kumwona kwa macho yake. Malaika alipofika kwa Anna alimwambia. "Sala zako zimekubaliwa na Mungu", Joakimu atakuwa Mume wako, usimkatae atakapofika kukutaka uchumba. Na ndoa ikifungwa muendelee kusali mkimwomba Mungu bila kuchoka na Masiha atazaliwa. Msichana huyu Mtakatifu licha ya kuwa mcha Mungu sana alikuwa na sifa zingine nzuri.

Alikuwa na sura nzuri ya kuvutia, bahati ya kujua na kujulishwa mambo mengi ya Mungu kwa njia ya Malaika kuliko Joakimu. Baada ya Anna kujulishwa habari hizo, ilipofika usiku wa siku hiyohiyo. Joakimu akiwa amelala usingizi mnono; Malaika Gabriel alimtokea katika ndoto akamwambia "Anna atakuwa Mke wako nenda kamchukue". Joakimu alipoamka asubuhi alifunga safari kwenda Betheremu nyumbani kwao Anna. Akamchumbia na kufanya mipango ya ndoa. Siku chache baadaye walifunga ndoa wakawa Mume na Mke.

MAISHA YA NDOA NYUMBANI KWAO NAZARETI

Watakatifu hawa baada ya kufunga ndoa yao walienda kuishi mjini Nazareti – Galilaya nyumbani kwa Joakimu. Walidumu katika kumcha Mungu kwa sala, furaha na mapendo makubwa ya ndoa yao. Licha ya kuwa na nyumba kule Nazareti – Galilaya walikuwa na nyumba ndogo kule Yerusalem. Karibu na lango la ukuta wa Hekalu kuu. Kutoka Nazareti mpaka Yerusalem ni umbali wa maili 68 au Km 109.5 kwa kutembea kwa miguu, lakini kwa gari ni umbali wa maili 94.5 au Km 152.8 na ukitumia usafiri wa ndege ni maili 63 au Km 101.4 Mungu aliwajalia na kuwabariki. Walikuwa na utajiri mwingi wa Mali. Walikuwa na mashamba makubwa na mifugo mingi, kweli walikuwa na kila kitu cha kuwafanya wawe na furaha duniani.

TABIA ZAO

Joakimu alipenda kufanya kazi ya kutunza mashamba na kuchunga mifugo yao kwenye milima ya Galilaya. Naye Anna alipenda sana kumtunza mume wake na nyumba yao. Kwa ujumla mama huyu alipenda sana kazi za nyumbani.

Kutokana na mazao ya mashamba na mifugo yao walipouza walipata fedha nyingi. Na mapato yao waliyatumia katika sehemu tatu. Kwanza waliwagawia masikini, Pili walitoa zaka na sadaka Hekaluni na Tatu walitunza kwa ajili ya chakula chao na mahitaji mengine.

JOAKIMU NA ANNA WANAKASHIFIWA NA MAJIRANI

Katika miaka ishirini (20) waliyoishi ya Ndoa yao yenye kupendeza na kuvutia na kuwa mfano wa kuigwa na jirani zao, Mungu hakuwajalia kupata mtoto hata mmoja. Hali hii wao wenyewe walijisikia wanyonge na wakiwa sana; kwa kukosa mtoto wa kuwachangamsha. Zaidi sana kutokana na kabila la Kiebrania, familia isiyokuwa na mtoto hudhaniwa kuwa haina Baraka za Mungu. Hivyo watu walioishi nao jirani waliwadharau sana na kuwatukana, kwa kuwakashifu kwamba walikuwa wagumba na hawakuwa na thamani kwa Mungu. Hata Masiha akija walifikiri kwamba hawatakombolewa.

Lakini pamoja na kashifa zote hizo na kudharauliwa namna hiyo wao hawakujali, ila walimshukuru Mungu na kumwomba sana awajalie kupata mtoto ili waweze kupumzika na dharau na matusi ya watu; hasa ya jirani zao. Katika kuomba kwao Mungu awape mtoto, Joakimu na Anna walimwahidi Mungu kuwa wakipata mtoto huyo awe wa kiume au wa kike watamtolea kwake Mungu ili awe mtumishi wake Hekaluni. Waliamini pia kuwa maombi na dua zao Mungu atazipokea na siku moja atawatendea mambo makuu ya ajabu, mpaka jirani zao wataaibika. Kama tusomavyo katika "Yeremia 33:3, 9 Niite, name nitakuitikia, name nitakuonesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua. Na mji huu utakuwa kwangu jina la furaha, na sifa na utukufu, mbele ya mataifa yote ya dunia, watakaposikia habari ya mema yote niwatendeayo, nao wataogopa na kutetemeka, kwa sababu ya mema yote na Amani nitakayoupatia mji huo."

JOAKIMU ANAFUKUZWA HEKALUNI

Siku moja Joakimu na jamaa zake walienda Hekaluni kusali na kutoa sadaka kwa ajili ya kumuomba Mungu Masiha aje haraka pia kumwomba Mungu awajalie Joakimu na Anna kupata mtoto. Lakini ilitokea humo Hekaluni mambo ya ajabu ambayo Joakimu na jamaa zake yaliwastaajabisha na kuwatia uchungu sana.

Kwani Joakimu alipambana na kuhani msaidizi aliyejulikana kwa jina la Isaack ambaye alikuwa anawafahamu Joakimu na mke wake Anna kuwa ni matajiri wa Mali na mifugo pia ni wacha Mungu lakini hawakuwa na mtoto hata mmoja. Yule Kuhani alimwendea Joakimu mahali alipokuwa ameketi humo Hekaluni wakisali yeye na jamaa zake, akamnyanyasa kwa kumwambia.

"WEWE JOAKIMU KWANINI UMEKUJA HAPA KUMCHUKIZA MUNGU, WEWE HUNA MTOTO HATA MMOJA UNAKUJA KUFANYA NINI? TOKA HUMU HEKALUNI UENDE ZAKO. HUJUI KUWA HIZO SALA NA SADAKA ZAKO HAZINA THAMANI MBELE ZA MUNGU? WEWE NI MGUMBA, MTU USIYEFAA KABISA, ONDOKA HUMU HEKALUNI SASA HIVI. USIZIDI KUMCHUKIZA MUNGU KWA HIZO SALA NA SADAKA ZAKO."

Basi Joakimu akiwa na aibu kubwa ya Moyo na mwili alifadhaika mno na akapata uchungu mkali kwa maneno hayo. Kabla ya kuondoka humo Hekaluni baada ya kufukuzwa na huyo Kuhani msaidizi alisujuduu na kumwomba Mungu akisema. "Mungu wangu kwa amri na mapenzi yako nimekuja Hekaluni, lakini huyu aliyechukua nafasi yako hekaluni ananinyanyasa, nami kutokana na dhambi zangu nastahili aibu hii. Basi nakuomba Mungu wangu usinitupe mimi kiumbe chako dhaifu" mara baada ya sala hiyo akaondoka haraka. Kutokana na aibu hiyo aliyoipata hakupenda hata kurudi nyumbani kwake, bali aliondoka upesi akaenda moja kwa moja mpaka kwenye mashamba yake ambako kulikuwa na ghala kubwa la kutunza mazao yao. Jamaa zake aliwaacha humo humo hekaluni, ila yote aliyotendewa na huyo kuhani msaidizi waliyashuhudia. Nao walisikia uchungu kuona jamaa yao alivyotendewa. Basi Joakimu alipofika huko shambani akaingia ghalani akasali akasema.

"Mungu wa Ibrahim, Mungu wa Yakobo, Mungu wa Isaack wewe umewasaidia vizazi na vizazi na umetupa mwongozo wako ukisema yeyote atakayeomba kwa Imani utamsaidia. Mimi sasa nakuomba kwa Imani. Nakuomba upokee sala zangu na za mwenzangu Anna. Utupe mtoto. Na kama umetuona kuna kitu kinachozuia tusipate mtoto, tunakuomba sasa ukiondoe. Ninazidi kukuahidi kuwa mtoto tutakayempata tutamtolea kwako awe mtumishi wako Hekaluni".

Wakati Joakimu anasali sala hiyo huko shambani, Anna mkewe kwa kipindi hicho hicho nae alikuwa anasali nyumbani kwake. Aliomba Mungu awajalie kupata mtoto. Wala hakujua mkasa uliokuwa umempata mume wake.

Sala aliyosali Anna ni hii.

"Mungu wangu kumbuka wewe ulimpatia Anna somo yangu mtoto ambaye naye alikuwa Mgumba, nakuomba kwa huruma yako na mapenzi yako unijalie na mimi kupata mtoto rejea (1 Samweli 1:1-20)"

MALAIKA GABRIEL ANAWAPASHA HABARI NJEMA

Kilio na sala za Watakatifu hawa zilimfurahisha Mungu. Hasa kwa jinsi walivyokuwa wanyenyekevu wa moyo. Mara baada ya sala hizo Mungu alimtuma Malaika Gabriel akamtokea Anna na kumjulisha kwamba sala zake zimepokelewa na Mungu, hivyo atapata mtoto. Mama huyu aliposikia habari njema hiyo alijawa na furaha kubwa sana isiyoelezeka. Alichekacheka peke yake halafu akamshukuru Mungu.

Malaika alipomaliza kumpasha habari hiyo Anna. Akaondoka mpaka shambani alikokuwa Joakimu amekimbilia baada ya kufukuzwa Hekaluni na Kuhani Msaidizi. Malaika alipofika akamtokea Joakimu ambaye alikuwa na mawazo mengi kwa yale yaliyompata kule Hekaluni. Malaika akasema Joakimu usiogope mimi niliyesimama nawe ni Malaika Gabriel nimetumwa na Mungu kuja kukujulisha habari njema za furaha kuu kwako na kwa mke wako. Sala zako zimekubaliwa na kupokelewa na Mungu. Na kwamba Mke wako atapata mimba atamzaa mtoto wa kike na utampa jina la MARIA lenye maana ya Nyota ya Bahari, Mwangaza na Bibi. Mtoto huyu amebarikiwa kuliko wanawake wote (Luka 1:41-42) Baadae atakapozaliwa kama mlivyoahidi ninyi wenyewe, wewe na mke wako mnapaswa kumtolea mtoto wenu Hekaluni. Lakini Malaika alimficha Joakimu hakumwambia kama mtoto huyo atakuwa mama wa Masiha.

Baada ya Joakimu kusikia habari hiyo njema kutoka kwa Malaika. Naye alijawa na furaha kubwa sana ya ajabu, hata alikaribia kufa kwa furaha hiyo aliyopata. Lakini Mungu alimkinga kifo kisimpate. Kwa furaha hiyo mara alisahau yale yote yaliyompata kule Hekaluni pamoja na kashifa za jirani zake. Akamtukuza Mungu kwa shangwe moyoni mwake. Kasha Malaika akamwambia tena ili kuthibitisha habari hii njema rudi tena hekaluni ukasali na kumtolea Mungu sadaka ileile iliyokataliwa na Kuhani aliyekufukuza hiyo ndio shukrani kwa Mungu kwa kuwa amekuahidi kupata mtoto. Na utakapofika huko yule Kuhani hatakufukuza tena, na pale Hekaluni utakutana na mke wako kama ishara nyingine ya haya niliyokueleza kuwa Mungu amenituma kwako. Baba huyo Mtakatifu kwa furaha kuu hakuchelewa alikimbia mbio kurudi tena Hekaluni ili akathibitishe aliyoambiwa na Malaika.

Alipofika Mlangoni mwa Hekalu kweli alikutana na Mke wake, wakakumbatiana kwa furaha kuu, wakaingia wote Hekaluni wakamshukuru Mungu na kumtolea sadaka zao. Wakarudi nyumbani, siku si nyingi Anna akashika ujauzito.

ANNA ANAPAMBANA NA MISUKOSUKO YA SHETANI

Joakimu na Anna walichaguliwa na Mungu kuwa wazazi wa Bikira Maria kwa vile walikuwa na utakatifu wa hali ya juu sana kuliko Mwanadamu yeyote aliyewahi kuishi wakati huo. Naye Bikira Maria alikuwa na Utukufu Mkuu na Utakatifu kupita viumbe vyote vilivyowahi kuumbwa hapa duniani wala huko mbinguni. Mungu aliona ni vema azaliwe na wazazi hawa Watakatifu. Furaha ya Joakimu na mkewe Anna na jamaa zao iliendelea kuwa kubwa na mimba ya Mama Anna iliendelea kukua. Waliendelea kumwomba Mungu mtoto azaliwe salama. Lakini palipo furaha hapakosi machukizo. Ndipo mlaanifu Shetani na wafuasi wake walivyochukia kuona Mama huyu Mtakatifu na jamaa zake walivyoonesha furaha yao na kusahau machungu ya matusi na manyanyaso ya jirani zao.

Shetani na wafuasi wake siku zote waliogopa Utabiri wa Manabii juu ya kuja kwa Masiha ili kuikomboa dunia kutoka mikononi mwake. Ni wazi kwamba Shetani hakupenda kabisa Mama wa Mungu azaliwe au Masiha aje duniani. Shetani alipata hofu sana alipomwona mama huyu mcha Mungu ni mjamzito, alihisi kuwa pengine atamzaa Masiha au Mama wa Masiha, hivyo Shetani na wafuasi wake wakapanga mbinu za kumwangamiza Mama huyo kabla ya siku ya kuzaa kwake, ama wamuue mtoto akiwa tumboni au mara baada ya kuzaliwa. Lakini fikra, mbinu na mipango ya shetani kwa Mungu ni sawa sawa na ndoto za mwendawazimu. Mungu alijua mipango yote hiyo ya shetani mapema. Mungu akamwekea Anna ulinzi wa kundi kubwa la Malaika ili wamlinde mama na mtoto atakayezaliwa, mimba ikaendelea kukuwa na miezi ya kuzaa kwake ikakaribia. Shetani na wafuasi wake walipojaribu kutekeleza mipango yao wakashindwa. Ndipo walipotambua Mama analindwa na jeshi kubwa la Malaika toka mbinguni. Hapo wakazidi kupata wasiwasi mwingi zaidi kuwa atakayezaliwa pengine atakuwa Masiha aliyetabiriwa, au atazaliwa Mama wa Masiha. Shetani akawaambia wafuasi wake kuwa Mama huyu ana ulinzi mkubwa sana, Hivyo kazi ya kumwangamiza Mama ataifanya yeye mwenyewe.

SHETANI ANAANZA MAPAMBANO

Mbinu ya kwanza ya Shetani ilikuwa kuiangusha nyumba waliyokuwa wakiishi Joakimu na mkewe Anna, ili iwaangukie na kuwaua wakati wakiwa wamelala usingizini. Usiku mmoja Shetani alienda jirani na nyumba hiyo akafanya kishindo kikubwa na tetemeko la ajabu. Akasukuma nyumba kwa nguvu zake zote; lakini alishindwa. Malaika walinzi waliotumwa kumlinda mama na mtoto waliizuia nyumba isianguke, hivyo mbinu ya kwanza ya shetani ikashindwa.

SHETANI ANAJIGEUZA MSICHANA

Siku iliyofuata Shetani alifikiria mbinu nyingine, nayo ni kujifanya binadamu. Alijigeuza kuwa Msichana mzuri, mrembo wa kuvutia kwa sura tena mnyenyekevu mwenye nidhamu ya hali ya juu. Akaenda kuomba kazi za nyumbani kwa Joakimu na Anna. Kutokana na kukuwa kwa mimba Anna alihitaji msichana wa kumsaidia kazi. Kipindi hiki alikuwa amechoka, hakuweza kufanya kazi ngumu. Kwa jinsi alivyoonekana hakuna mtu aliyeweza kumtambua kuwa alikuwa shetani, watu wote walimwona sawa na watu wengine. Hata Joakimu na Anna hawakumtambua alipofika kuomba kazi. Shetani alipofika akawasalimu na kujieleza kuwa anaomba kazi za ndani. Yeye ni msichana ambaye bado hajaolewa. Tena ni fukara na wazazi wake walifariki siku nyingi. Hana chakula wala mahali pa kuishi, anatangatanga na maisha ni ya taabu sana, kwa maelezo hayo Joakimu na Mke wake wakamwonea huruma, wakamwajiri.

Anna alifurahi kupata msichana wa kumsaidia kazi za nyumbani katika kipindi hicho cha ujauzito. Msichana Shetani akakaribishwa na kupatiwa chumba cha kulala na siku iliyofuata akaanza kazi. Siku za mwanzo alionesha tabia ya upole, unyenyekevu, heshima na tena mchapa kazi hodari. Mzee Joakimu na Mkewe wakampenda sana msichana huyu. Lakini Shetani ni shetani tu. Kadri alivyozidi kuishi pale nyumbani tabia yake ilianza kubadilika, akaanza kuwa kiburi na matusi yenye kashifa kama zilizokuwa zinafanywa na jirani zake Joakimu na Anna. Lakini familia hii Takatifu bila kujua walimkaribisha shetani, waliendelea kumpenda na kumuombea kwa Mungu ilia ache tabia hizo mbaya.

Basi siku moja Msichana shetani alipanga kutimiza mpango wake wa kumwangamiza Mama na Mtoto. Akaazimia kumwekea sumu Anna katika chakula au kinywaji. Mungu akamwonea huruma Anna. Akawaamuru wale malaika walinzi kumfukuza Msichana Shetani. Malaika wakamfukuza. Joakimu na Anna walishangaa kuona msichana wao wa kazi ametoweka ghafla bila kuaga.  Ndipo walipogundua kuwa hakuwa binadamu wa kawaida bali walikuwa wamemkaribisha shetani. Hata hivyo Shetani hakuchoka kuja mara kwa mara kujaribu mbinu mpya za kumwangamiza Mama na mtoto tumboni, lakini alishindwa kwa  kuwa Malaika walinzi waliimarisha ulinzi mkali siku zote.

BIKIRA MARIA ANAZALIWA

Hata siku ya kumzaa Bikira Maria ilipofika, Mungu alimjulisha Anna katika mawazo kuwa muda wa kujifungua mtoto umefika. Kwa vile alikuwa ameomba kwa Mungu kwamba Mtoto anapozaliwa asishikwe na mtu yeyote. Ili kuonesha ombi lake lilikuwa limekubaliwa na Mungu, muda wa kujifungua mtoto ulipofika, Mume wake alipewa usingizi mzito asiweze kumwona mtoto wakati wa kuzaliwa kuzaliwa kwake. Japo walikuwa pamoja chumbani. Tena Mungu alimkinga Mama asipate uchungu wa kuzaa kama desturi. Mtoto alipozaliwa alipokelewa na Malaika.

Mungu kwa kupitia Malaika, Anna alijulishwa kuwa mtoto aliyezaliwa anapaswa kulelewa kama watoto wengine. Lakini apewe heshima ya pekee kwa kuwa atakuwa mama wa Mungu. Heshima hiyo aiweke moyoni mwake wala asioneshe kwa watu wengine, Malaika Makundi kwa makundi walishuka kutoka mbinguni. Hesabu yao haijulikani. Wakajumuika na wale Malaika walinzi. Huku wakiimba nyimbo nzuri na kumsifu Mungu. Zilikuwa nyimbo nzuri za kumsifu Mungu, zilikuwa nyimbo za kuvutia sana. Anna alijaliwa kuwaona Malaika na kuyaona mambo yote wazi wazi kwa macho yake yaliyofanyika na kusikia nyimbo za Malaika. Kwa furaha kuu akamshukuru Mungu kwa kumpata mtoto.

Baada ya kujifungua ndipo alipomwamsha Mume wake. Joakimu alishangaa kuona Mke wake amepata mtoto bila mkunga yeyote wa kumsaidia. Kwa furaha alipiga magoti na akasujudu. Wote kwa pamoja wakasali, wakamshukuru Mungu, wakiwa na furaha ya ajabu isiyoelezeka. Furaha ilikuwa kubwa sana kupita hata ile ya kwanza walipopashwa habari na Malaika juu ya kupata mtoto. Hakika ilikuwa shangwe kuu. Joakimu akamchukua mtoto mikononi mwake akamtolea kwa Mungu ili kutimiza ahadi yao. Mtoto alizaliwa saa 6:00 usiku, tarehe 8 September. Hivyo ndivyo alivyozaliwa Mtoto Maria Mtakatifu na maajabu yake. Kanisa Katoliki huadhimisha sikukuu ya kuzaliwa Bikira Maria tarehe 8 September ya kila mwaka.

Kesho yake asubuhi watu wengi walifika nyumbani pale. Kumsalimu mtoto na kuwapongeza wazazi hawa. Watu wote waliofika walikuwa na furaha kubwa. Walileta mikononi mwao zawadi nyingi za aina mbalimbali zenye kuvutia. Siku ya nane wazazi hawa walimpa jina mtoto wao akaitwa Maria. Siku hiyo Joakimu alitayarisha sherehe kubwa sana. Watu wengi walihudhuria wakiwemo ndugu, jamaa na marafiki. Pia walikuwepo wale jirani zao waliokuwa zamani wakiwatolea kashifa na matusi. Malaika wa Mungu nao walihudhuria. Walikuwa wengi sana. Waliimba nyimbo zao nzuri za kumsifu Mungu. Anna peke yake aliendelea kuwaona na kusikia nyimbo hizo za Malaika. Lakini Mume wake na watu wengi wengine hawakujaliwa bahati ya kuwaona wala kusikia nyimbo zao. Siku hiyo ilikuwa ya furaha kubwa mno. Watu walikula na kunywa hata kusaza. Walimshukuru na kumtukuza Mungu mkuu. Wakiwaombea Baraka za Mungu, wazazi hawa na mtoto wao. Tangu siku hiyo wazazi hawa walianza kuheshimiwa na kuthaminiwa kama watu wengine wenye watoto katika kabila lao.

Joakimu na Anna wakaishi sasa kwa Amani na furaha kubwa katika ile jamii iliyowazunguka. Wakamlea mtoto wao katika kweli na haki. Huku wakiomba Masiha aje haraka.

MAISHA YA BIKIRA MARIA AKIWA MTOTO

Bikira Maria akiwa Mtoto alikuwa mchangamfu sana. Alipenda ukimya, hakupenda kulialia au kudeka kama walivyo watoto wengine kwa wazazi wao. Kwa tabia hiyo watu wengi walimpenda sana, hata yeye mwenyewe aliwapenda sana watu wote waliofika nyumbani kwao na kumpakata. Jambo lililowashangaza wazazi wake na watu wengine mtoto huyu wakati alikuwa bado hajaweza kukaa chini peke yake wala kusema; lakini alionekana ana hekima kama mtu mzima, alikuwa anaelewa kila kitu kinachosemwa au kutendwa. Mtoto Maria alikuwa ana ulimi mzito hakuweza kuongea mapema, mpaka alipotimiza umri wa Mwaka mmoja na miezi sita ndipo alipoanza kuongea. Wazazi wake na watu wengine walidhani pengine angekuwa bubu.

Alipotimiza umri wa miaka miwili, Mama yake alianza kumfundisha kusoma na kazi nyepesi.

Aliongozana naye kwenda kutoa misaada kwa masikini. Tabia hii mtoto Maria ilimfurahisha sana, aliipenda na kuizoe haraka. Kila mara walipofika pale kwa masikini Mama yake alimzoesha kumpa Mtoto zawadi walizokuwa wamekuja nazo ili awagawie masikini. Halafu alimfundisha baada ya kuwagawia zawadi, kuwabusu wale masikini mikono na miguu yao. Kuna wakati Fulani Mtoto aliwagawia masikini nusu ya chakula chake alichopewa siku hiyo kula yeye mwenyewe jambo ili pia liliwastaajabisha sana wazazi wake. Siku zilipozidi mtoto alizoea kazi hii. Mwisho alikuwa anakwenda peke yake kuwahudumia wale masikini.

Zipo siku alizokwenda kuwapelekea zawadi wale masikini akawakosa. Mtoto alisikitika sana moyoni kuwakosa rafiki zake wapenzi, kwa heshima ya rafiki zake hawo aliamua kubusu ardhi eneo walilopendelea kukaa ama kupita wale masikini.

BIKIRA MARIA NA WAZAZI WAKE WANAONA MAONO

Mtoto Maria akiwa na wazazi wake nyumbani kwao Nazareti, kwa pamoja walikuwa wameketi sebreni. Ghafla waliona maono ya Utatu Mtakatifu ambao ulimwambia mtoto huyu Mtakatifu kuwa inampasa kujitolea mwenyewe kwa Mungu ili awe Mtumishi wa Hekaluni. Pia Utatu Mtakatifu uliwakumbusha wazazi wake kuwa siku zimekaribia za kumtolea mtoto wao kwa Mungu Hekaluni kama walivyoahidi kabla ya kuzaliwa mtoto huyu.  Mama yake Maria aliposikia habari hiyo alijisikia uchungu mkubwa wakutengana na binti yao waliomzoea na kuwachangamsha. Mungu aliuona uchungu wa Mama huyu akamuonea huruma akampoza machungu yake.

BIKIRA MARIA ANATOLEWA KWA MUNGU HEKALUNI

Siku zilienda mbio, mtoto alipotimiza umri wa miaka mitatu. Wazazi hawa Watakatifu walipanga safari ya kumpeleka mtoto wao hekaluni, ili kumtolea kwa Mungu kama walivyohaidi. Siku ilipofika Mama alimbeba mtoto akiongozana na Mume wake. Safari hiyo ilikuwa ndefu walitoka Nazareti kwenda Yerusalemu umbali wa maili 68 kwa kutembea kwa miguu lakini ilikuwa safari ya furaha kwa wazazi hawa na mtoto wao. Kundi kubwa la Malaika wa Mungu liliwasindikiza, Mtoto Maria aliwaona Malaika hao. Ila wazazi wake walifumbwa macho na Mungu hawakuweza kuwaona Malaika.

Walifika salama Yerusalemu, katika viwanja vya Hekalu, Mama akamtelemsha Mtoto. Kwa mapendo makubwa wazazi wote wawili wakamshika mikono mtoto wao, mmoja kulia na mwingine kushoto. Mtoto akawa katikati ya Baba na Mama yake wakatembea polepole kuelekea jingo la Hekalu kuu, walipofika lango kuu wakaingia ndani pamoja, wakapiga magoti, humo hekaluni walimkuta kuhani Mkuu akisali. Joakimu na Anna wakasali sala ya kumtolea mtoto kwa Mungu na Mtoto Maria akasali sala yakujitolea yeye mwenyewe kwa Mungu. Baada ya sala zao kukasikika sauti ya upole ndani ya jengo lote la hekalu iliyosema.

"KARIBU MCHUMBA WANGU MPENZI, KARIBU HEKALUNI MAHALI AMBAPO NAPENDA KUSIKIA SAUTI YAKO NZURI YA KUNISIFU". Sauti waliisikia watu wote waliokuwemo Hekaluni. Baada ya sala wazazi na mtoto waliinuka walipokuwa wamepiga magoti wakamuongoza mtoto mahali alipokuwa ameketi Kuhani Mkuu Simoni wakamkabidhi mtoto wao.

Kuhani Mkuu akampokea mtoto. Halafu akawaongoza wazazi na mtoto mpaka kwenye nyumba ya malezi, walipokuwa wanalelewa Mabinti wote wa ukoo wa Yuda na Lawi mpaka walipofikia umri wa kuolewa ndipo waliruhusiwa kurudi makwao au waliopenda walibaki pale kwa maisha ya kitawa, nje ya jengo hilo walimkuta Kuhani mdogo amesimama kwenye ngazi za kwendea langoni, jengo hilo lilikuwa na ngazi kumi na tano za kupanda kabla ya kufikia mlango wa kuingia. Kuhani mdogo akawapokea akambeba mtoto ili kumpandisha kwenye ngazi, alihofia akipanda peke yake pengine angeweza kudondoka chini kwasababu ya ulefu wa ngazi hizo.

Kutokana na sheria za nyumba ya Malezi, haikuruhusiwa kuingia ndani ya nyumba ya malezi mtu yeyote asiyekuwa mtumishi au mlezi wa mabinti hao. Hivyo kuhani mdogo alimsimamisha mtoto kwenye ngazi ya kwanza ili awaage wazazi wake. Mtoto Maria alipiga magoti kuwaelekea wazazi wake. Halafu akaomba Baraka zao, wazazi wake wakambariki naye akabusu mikono yao.

Baada ya kupata Baraka, mtoto Maria bila yakujali au kuonesha uchungu wakutengana na wazazi wake tena bila kusubiri kuongozwa au kubebwa tena kuhani mdogo; yeye mwenyewe kwa haraka aliparamia zile ngazi mpaka akaufikia ule mlango wa kuingilia. Akapiga hodi na kuingia ndani, wakati huo wazazi wake pamoja na Makuhani walikuwa bado wapo pale nje, walishangazwa kuona ujasiri wa Binti huyu.

Makuhani wakasema hawajawahi kuona ujasiri mkuu wa namna hiyo kati ya Mabinti wote waliowai kupokelewa pale baada ya maongezi hayo, Joakimu na Anna wakaagana na Makuhani wakarudi nyumbani kwao kwa furaha.

BIKIRA MARIA KATIKA NYUMBA YA MALEZI

Mtoto Maria baada ya kufunguliwa mlango na kuingia katika nyumba ya Malezi, Mabinti wenzake waliokuwa wanalelewa humo pamoja na Mama walezi walimpokea kwa furaha na mapendo makubwa. Kuhani Mkuu Simoni alimteua Mama mmoja awe mlezi wa mtoto huyu ambaye alijulikana kwa jina la Anna jina la Mama huyu lilifanana na jina la Mama mzazi wa Maria. Mama huyu alikuwa na sifa ya kutabiri mambo yajayo. Mama huyu alikubali kuwa mlezi wa mtoto huyu kama alivyoteuliwa na Kuhani Mkuu.

Mtoto Maria alipotambulishwa kwa Mama mlezi wake alifurahi sana, akachukua vitu alivyotoka navyo nyumbani, zikiwemo pesa na nguo zake akamkabithi mlezi wake ili awagawie masikini. Yeye alibaki na vitu vichache tu, na nguo alizokuwa amevaa. Basi jambo hili liliwastajaabisha Sana wenzake pamoja na walezi wao. Kwa hali hiyo akaonekana Binti masikini kuliko wote. Hata baadhi ya mabinti wenzake walivyoona hivyo palepale wakaanza kumdharau mioyoni mwao.

Usiku ulipoingia bila mtu yeyote kujua, mtoto Maria alichukuliwa na Malaika mpaka mbinguni mbele ya Utatu Mtakatifu. Alipofika huko akaahidi kuwa atakuwa mtawa maisha yake yotekatika nyumba ya malezi.

Siku iliyofuata mama mlezi wake alianza kazi yake ya kwanza ya kumfundisha sheria za kitawa .nazo zilikuwa tatu .kwanza utii, pili umasikini na tatu usafi wa roho na mwili.baada ya siku chache kuhani mkuu akamwapisha .naye akaweka nadhiri ya kuishi kitawa kwa maisha yake yote mpaka kufa.

TABIA YA MTOTO MARIA KATIKA NYUMBA YA MALEZI.

Maisha ya utawala ya mtoto huyu katika nyumba ya malezi yalianza vizuri bila matatizo yoyote.mama mlezi wake alimuongoza vizuri, alipenda maandiko matakatifu kwa kujisomea na kufanya kazi nyingine kadiri alivyoelekezwa.

MARIA ANALETEWA TAARIFA YA KIFO CHA BABA YAKE

Baada ya miezi sita kupita, Mungu aliwatuma Malaika wamjulishe kuwa Baba yake mzazi atakufa muda mfupi ujao. Mtoto alimshukuru Mungu kwa kumpelekea habari hiyo. Taarifa haikumtia hofu wala masikitiko kwakuwa alijua kila mwisho wa maisha ya binadamu ni kifo.

Akamuomba Mungu kupitia wale Malaika amjalie Baba yake afe kifo chema, walezi wa Maria nao walipelekewa taarifa ya kifo cha Mzee Joakimu, lakini Maria hawakumruhusu kwenda kumzika Baba yake kwa vile walitaka kuona kama anaiweza ile amri ya kitawa ya kuwa mtii kwa viongozi wake.

Maria alikuwa akilindwa siku zote na Malaika kumi na wawili. Na alikuwa akiwaona akawaruhusu hao Malaika walinzi wake waende kumlinda Baba yake na Mashambulio ya shetani saa ya kufa.

Mungu alifurahishwa sana na maombi ya  Maria pia kuwaruhusu wale Malaika walinzi wake waende kumlinda Baba yake, Mungu akatuma jeshi kubwa la Malaika nao wakajumuika na wale Malaika walinzi wakaenda kumlinda mzee huyu Mtakatifu. Malaika walipofika kwa mzee Joakimu, Mungu akamfunulia macho akawaona hao Malaika kwa macho yake. Nao Malaika wakamjulisha kuwa wametumwa na Binti yake kwa ruhusa ya Mungu waje kumlinda dhidi ya mashambulio ya shetani katika saa yake ya mwisho. Mzee alifurahi sana akamshukuru Mungu na mwanaye kwa fadhila hiyo kuu. Maria alijua pia kuwa Mungu amewatuma idadi kubwa ya maelfu ya Malaika ya kumlinda Baba yake. Naye alifurahi sana na kumshukuru Mungu.

Mzee Joakimu dakika chache kabla ya kufa alifunuliwa na Mungu ile siri aliyoambiwa Mke wake siku aliyozaliwa mtoto wao, kuwa "Mtoto wao alikuwa Mama wa Masiha aliyetabiriwa na manabii, na kwamba amebarikiwa kuliko wanawake wote na Ukuu wake ni wa pili kutoka kwa Mungu." Mzee alifurahi sana moyoni mwake akatabasamu, akamshukuru Mungu, halafu akakata roho akiwa amelala kitandani. Mke wake akiwa karibu naye amesimama upande wa kichwani mwa kitanda. Alikufa kifo kitakatifu chenye furaha yakumuona Mungu. Baada ya kifo cha mzee huyu, Mke wake alitoka akawajulisha majirani zao. Ndugu na jamaa walifika wakamlilia Baba huyu Mtakatifu. Mwili wake ukazikwa kama ilivyo desturi na mila zao. Roho yake ikachukuliwa na malaika ikapelekwa limboni.

BIKIRA MARIA ANAJARIBIWA NA SHETANI

Shetani aliona Mzee Joakimu analindwa na kundi kubwa la Malaika kabla ya kufa na hata wakati wa mazishi yake, kwasababu hiyo hakuweza kumshambulia hata kidogo. Akakasirika sana, hivyo akamuomba Mungu ruhusa aende nyumba ya Malezi akamshambulie mtoto Maria ili amtukane Mungu apate kufukuzwa Utawani. Mungu alikubali akamruhusu Shetani akaenda katika nyumba ya malezi, alipofika huko jaribio la kwanza lilikuwa kumfumba macho asiweze kuwaona wale malaika wa Mungu waliokuwa wakimlinda, wala hakuweza kusema nao hali hiyo ilimshtua sana, ikampa uchungu moyoni. Tena akajisikia mpweke alifikiri na kujihoji akilini kwanini hali hii imetokea hivi? Akawaza kuwa pengine amemkosea Mungu kwa namna flani ndio maana macho yake yamefumbwa asiwaone tena Malaika na kuongea nao.

Siku zilizivyozidi akafumbwa zaidi hata hakuweza kumuona Mungu tena kama zamani, hali hiyo ilimzidishia uchungu na mawazo mengi moyoni.

Bikira Maria hakujua hizo zilikuwa mbinu za shetani, akahuzunika sana moyoni.

Akaanza kumuomba Mungu wale Malaika wamjulishe kama kuna jambo amekosea ili amuombe toba. Akasali akasema "Mungu wangu mimi najiona mdogo kuliko viumbe vyote vilivyoko mbinguni na duniani. Japo umeniachia vinitulize lakini mimi sivitamani hata kidogo natamani tu Mungu wangu kukuona wewe Mchumba wangu".

Katika nyumba ya malezi alipedwa sana na Makuhani, Mama walezi na mabinti wenzake kwasababu ya unyenyekevu, upole na heshima yake kwa watu wote. Ingawa baadhi ya wasichana wenzake walimdharau kwa vile alikuwa amebaki fukara bila nguo na vitu vya thamani baada ya kugawa vitu na nguo zake kwa masikini.

Jaribio la pili, Shetani aligundua kuwa Bikira Maria alikuwa anapendwa na watu wote. Akatafuta mbinu nyingine ili achanganyikiwe zaidi na halafu amtukane Mungu, Shetani na wafuasi wake wakawaingia wale wasichana wengine waliokuwa wakielewana naye. Mioyo yao ilijaa husuda wakaanza kumchukia sana na kumtukana wakisema; Maria mnafiki mpenda kujipendekeza kwa wakubwa tena mchongezi mkubwa. Lakini yeye alipotukanwa hakuwajibu neno lolote alinyamaza tu.

Wasichana hao walipoona hajibu neno lolote walianza kumchongea kwa wakubwa wao, Maneno ya uwongo ili afukuzwe napo wakashindwa.

Siku nyingine wasichana hao wakamchukua wakamuingiza katika chumba kimoja wapo kilichotumika kwa maongezi, kilikuwa chumba safi na chenye utulivu usioweza kupenyeza kelele yeyote ile, walipofika humo walianza kumtukana sana halfu wakampiga makofi, kelele zikawa nyingi mwisho mama walezi wakasikia wakaja mbio. Walipofungua mlango wa chumba hicho wakawakuta wale wasichana wamemvamia Maria wakimshambulia kwa maneno na kumpiga.

Wale wasichana walipoona wamegundulika na wakubwa wao, wakaanza kujitetea wakisema. Wapendwa Mama walezi wetu, Msichana huyu ni mtu mbaya sana. Tulikuwa kutiwaambia hamkumchulia hatua yeyote. Tazameni siku zote akiwa mbele yenu hujifanya mtu safi lakini tukiwa naye ni mtu mwenye matusi na fujo nyingi, hivyo leo tupo hapa ilikumfundisha adabu njema, tena mara nyingi tukimshauri yeye huwa hataki kutusikiliza au kufuata ushauri wetu pia wakati mwingine huwa anatupigia magoti ya kutuziaki akiomba tumsamehe halafu amekuwa mtu asiyetaka kubadili tabia yake. Uwongo huo wa wasichana hawa baada ya mama walezi kuhusikiliza kwa makini ukakubalika. Kwa vile yeye hakuweza kujitetea kutokana na kipigo alichopata kutoka kwa wenzake na kuendelea kumzomea. Shauri hili likawafikia Makuhani akapewa karipio kali na akatakiwa ajirekebisho vinginevyo atafukuzwa utawani.

Shetani alipoona hayo alifurahi sana, akazidisha mapambano vita hii ya shetani na Bikira Maria ilidumu kwa kipindi cha miaka saba kila siku kulitokea hili ama lile lililomhusu na kumuudhi au kumkosesha raha, siku nyingine tena wale wasichana wenzake walimshitaki tena kwa walezi wao walimsingizia kuwa Maria bado anaendelea na matusi na ukorofi wake hivyo akapendekezwa afukuzwe utawani. Makuhani wadogo na walezi waliposikia malalamiko hayo wakafanya mkutano kujadiri wafanye nini. Mwisho wa mkutano wao huo wote wakakubaliana kuwa Afukuzwe na arudishwe nyumbani kwao.

Katika kipindi chote alichokuwa akisingiziwa na kupigwa na wenzake, Maria siku zote alikuwa akimuomba Mungu ayaone mateso yake na amuhurumie pia aliwaombea sana adui zake na wakuu wake waweze kugundua fitina za adui zake. Maamuzi ya hao Makuhani na walezi ya kumfukuza utawani binti huyu yalipelekwa kwa Kuhani Mkuu Simon ili yapate Baraka zake. Kuhani Mkuu alipoyapokea akayabatirisha maamuzi haya akapendekeza apewe tena karipio kali sana. Binti huyu akaitwa na walezi wake akaonywa vikali sana.

Masikini Binti huyu alitoka kwa walezi wake akilia machozi kwa ajili ya maneno aliyoambiwa na walezi wake, kwani yalikuwa makali sana. Alipotoka nje wale adui zake walipomuona anakuja akilia walifurahi sana hata shetani alifurahi pia, ila hawakufurahi kuona hakufukuzwa utawani kwasababu hiyo wakapanga mbinu nyingine mpya na kubwa zaidi kuliko zote walizowai kuzifanya.

Chuki ikazidi sana kati yake na wale wasichana wenzake. Shetani akawapa mawazo mapya wakapagawa sana. Wakaitana na kufanya mazungumzo yao ya faragha bila kumshirikisha. Katika mazungumzo yao wakaadhimia wafanye mambo mawili. Kwanza kumfanyia mambo machafu ili kuharibu ubikira wake ili apatikane sababu ya kufukuzwa utawani. Pili au wamuuwe kwa kutumia njia yoyote watakayoweza na ambayo haitagunduliwa kwa makuhani na mama walezi.

MUNGU ANAINGILIA KATI

Mungu alipotambua nia mbaya za maadui wa Binti huyu akaingilia kati ili kumlinda Mtumishi wake mwaminifu. Usiku Mungu akawaotesha ndoto Mama Mlezi na Kuhani Mkuu Mungu akazungumza nao usingizini akasema. Maria ni Mtumishi wangu mwaminifu anayependeza machoni pangu kwa vile ni mwaminifu daima mashitaka yanayotolewa juu yake kwenu na wasichana wenzake yote sio ya kweli hata kidogo. Hata ilipofika asubuhi Kuhani mkuu na Mama mlezi wa Maria wakakutana na kusimuliana ndoto hiyo kila mmoja alivyoota. Wakagundua kuwa Mungu amesema nao usingizini. Wakaamua kumuita Binti huyu Mtakatifu na kumuomba msamaha kwa jinsi ya awali walivyomkaripia vikali. Naye akasema kwa unyenyekevu "Nasitahili maonyo yoyote kwa makosa yangu niliyofanya na nitakayofanya, tena nipo tayari kutii chochote mtakacho niamuru".

KIFO CHA ANNA MAMA MZAZI WA BIKIRA MARIA

Maria Bikira Mtakatifu alipotimiza umri wa miaka kumi na miwili (12) aliletewa taarifa na Malaika kuwa Mama yake Mzazi karibu atakufa. Binti huyu hakuweza kuwaona Malaika kwa macho walipomletea habari hii ya kifo cha Mama yake, kwani alikuwa bado amefumbwa ila taarifa hiyo aliipokea kwa kusikia sauti tu. Baada ya kupata taarifa hiyo alipiga magoti akamuomba Mungu akasema "Mungu wangu nakuomba umjalie Mama yangu afe kifo chema, kwani wewe wajua kuwa alikuwa mtumishi wako mwaminifu". Basi baada ya sala hiyo Mungu hakumjibu kwa maneno ila aliwaamuru wale Malaika waliokuwa wakimlinda wamchukue msichana huyu mpaka nyumbani kwao Nazareti akaonane na Mama yake kabla ya kufa. Wale Malaika wakamchukua bila ya mtu yeyote kujua wakampleka kama walivyoamuriwa na Mungu.

Malaika walipomfikisha nyumbani kwao akaonana na Mama yake, Mama yake alifurahi sana kuonana na Binti ye kwa mara ya mwisho. Maria pia alifurahi kuonana na Mama yake baada ya kutengana naye kwa muda wa miaka 9. Mtoto na Mama yake wakaagana. Maria akaomba Baraka ya mama yake, Mama akambariki Binti ye baada ya Baraka Mama huyu Mtakatifu akiwa na sura ya furaha akamuomba bintiye amfumbe macho baada ya kufa kwake. Muda mfupi Anna akiwa amelala kitandani kwake akakata roho.

Akafa kifo chema na kitakatifu, Mtoto akamfumba macho Mama yake kama alivyokuwa ameelekezwa. kule utawani alibaki Malaika Mmoja ambaye amejigeuza sura akaonekana kwa viongozi wa utawani na kwa watawa wengine kama Bikira Maria. Hivyo hawakuweza kugundua kama binti huyu Mtakatifu hayupo pale na kwamba amepelekwa Nazareti kuagana na mama yake.

MAZISHI YA MAMA YAKE

Jirani zake walipopata habari ya kifo cha mama huyu walikusanyika na wakautayarisha mwili wa mama huyu kama ilivyo desturi na kufanya mipango ya mazishi. Watu wengi walihudhuria msiba huu. Wakati watu walipouchukua mwili kwenda kuuzika, Malaika nao wakamchukua Bikira Maria na kumrudisha utawani. Akaendelea na shughuli za pale utawani kama kawaida huku akimshukuru Mungu kwa kuwatuma Malaika wampeleke kuagana na Mama yake na kushuhudia kifo chake. Lakini moyoni na akilini akawa na hisia kuwa wakati wa kuweza kumwona Mungu tena na wale Malaika uso kwa uso umekaribia. Akapiga magoti akasema. Malaika wangu wapenzi naomba mnijulishe lini nitawaona tena na kumwona Mungu kwa macho yangu. Nao Malaika wakamjibu wakasema; - utatuona hivi karibuni, muda wa kutuona na kumwona Mungu umekaribia mara baada ya maneno hayo ya Malaika; macho yake yakafumbuliwa, akauona Utatu Mtakatifu na wale Malaika kama mwanzo. Akafurahi sana, akamshukuru Mungu.

BIKIRA MARIA ANATOKEWA NA ROHO MTAKATIFU.

Mwaka mmoja na miezi sita baada ya kifo cha Mama yake wakati huo akiwa na umri wa miaka kumi na mitatu na miezi sita. Alitokewa na Roho Mtakatifu aliyetumwa na Mungu ambaye alimfahamisha kuwa kutokana na mapenzi ya Mungu, licha ya kuwa yeye ni Mtawa; lakini atapata mchumba na ataolewa. Tena mtoto atakayempata amtolee Hekaluni kama vile Nabii Ibrahimu alivyomtolea Mwanae Isaack kwa Mungu awe sadaka ya kuteketezwa. Msichana huyu alishangaa sana kupata ujumbe huu. Kasha akajisemea moyoni, itakuwaje jambo hili? Mbona mimi ni Mtawa na mtumishi wake Mungu Hekaluni!  Alijisemea hayo moyoni kwa sababu alikumbuka tangu alipokuwa na umri wa miaka mitatu alipoingia kwenye nyumba ya malezi, alijitolea kuishi kitawa mpaka kufa. Baada ya kutafakari hayo mara akajibu akasema. Bwana anitendee anavyotaka. Mungu akaahidi kumlinda na kila hila za Shetani na kwamba atakuwa nae siku zote. Kwa unyenyekevu mkubwa na upole, huku akiwa na hofu kubwa kwa mambo yajayo, akasubiri Mungu atakavyomtendea.

KUHANI MKUU NA MAMA MLEZI WANAOTA NDOTO.

Mji wa Yerusalemu wakati huo ulikuwa na mzee mmoja jina lake aliitwa Simoni, huyu ndiye yule Kuhani mkuu mwenye sifa kubwa ya kumcha Mungu, siku moja alitokewa na Roho Mtakatifu katika usingizi, akaota ndoto ya ajabu, ndoto hiyo ilimtaka afanye matayarisho ya kuolewa kwa Bikira Maria Mtawa. Binti wa Joakimu na Anna. Binti aliye mtumishi wa Bwana. Mwaminifu kwa Mungu na watu wote. Ndiyo ilikuwa sifa yake kwa wale watu waliopata kumfahamu wakati ule.

Kuhani Mkuu alipoamka akaikumbuka ndoto yake. Akashangazwa mno na ndoto hiyo kwa sababu alimjua binti huyu kuwa ni Mtawa. Lakini ghafla akiwa bado amezama na mawazo akilini na rohoni mwake kuhusu ndoto ile, Roho Mtakatifu akamtokea waziwazi. Akamwambia asiwe na wasiwasi wala asishangae kwani hayo ndiyo yalikuwa matayarisho ya kuja kwa Masiha aliyetabiriwa na Manabii. Basi Kuhani mkuu akiongozwa na huyo Roho Mtakatifu, akawaita Makuhani wote wa chini yake, wasomi mbalimbali pamoja na wavulana wote ambao wakati huo walikuwa bado hawajaoa, akawaeleza jinsi Mungu alivyomwongoza atangaze juu ya kumpata mtu atakayekuwa mume wa Bikira Maria Mtawa. Vijana walifurahi sana kusikia habari hii. Kwakuwa walikwisha sikia sifa nzuri za Msichana huyu. Kila mmoja alitamani awe Mume wa Binti huyu. Na katika vijana wote, alikuwepo kijana mmoja aliyekuwa naye amejitolea tangu utoto wake aishi maisha ya bila ndoa. (Maisha ya useja) kweli kijana huyu habari hii haikumfarisha hata kidogo, ndiye Yoseph (Mseremala) miezi sita ilipita baada ya vijana na Makuhani kupewa taarifa hiyo. Ndipo kuhani Mkuu alipowaita tena Hekaluni ili kufanya maombi na mafungo ili Mungu awaoneshe ni nani atakayekuwa mume wa Bikira Maria Mtawa. Wavulana wote wenye umri wa kuoa walifika. Humo Hekaluni Kuhani Mkuu aligawa fimbo kavu kwa kila kijana aliyehudhuria.

Naye Yoseph Mseremala alikuwepo, Kuhani Mkuu baada ya kuwagawia fimbo hizo akawafahamisha vijana hao kuwa fimbo itakayochipua ua jeupe, itakuwa utambulisho wa Mungu kuwa mwenye fimbo hiyo ndiye atakuwa Mume wa Bikira Maria Mtawa. Mfungo wa maombi yakaanza. Mafungo yalikuwa ya siku tisa. Katika maombi hayo Yoseph yeye aliomba Mungu amwepushe na hilo. Na kwamba amjalie neema ya kuishi kitawa mpaka kufa, akitunza usafi wa mwili na roho yake. Lakini mambo yakamgeukia, fimbo yake Yoseph pekee ilionekana imechipua ua jeupe. Ishara nyingine ilimtokea, njiwa mweupe alitua kichwani pake. Makuhani na wale wavulana wenzake waliokuwepo nae wakashuhudia, ikajulikana Yoseph amechaguliwa na Mungu kumwoa Bikira Maria mtawa. Akiwa ameshikwa na butwaa kuona fimbo yake ndiyo iliyochipua ua akatamani kukimbia mbio; akashindwa. Kuhani Mkuu akamtangaza rasim kuwa ndiye mteule wa Bwana atakayefunga ndoa na Maria mtawa. Wote waliokuwepo hekaluni wakamshangilia kwa vifijo na nderemo. Vijana wenzake wakampa mkono wa pongezi. Kati yao vijana wengine baada ya kuona hivyo waliondoka kwa shingo upande kwa kuwa hawakupata bahati ya kuchaguliwa, Makuhani nao walimpongeza sana Yoseph.

Kuhani Mkuu Simoni na Mama Mlezi Anna wakampa mkono wa pongezi Bikira Maria kwa kuonesha tabia nzuri katika maisha ya kitawa walimuomba msamaha kwa jinsi awali uongozi walivyokuwa wanampa hukumu ya makaripio na mashitaka ya uwongo yaliyosemwa na wasichana wenzake katika nyumba ya malezi ya utawa.

NDOA INAFUNGWA

Kuhani Mkuu akaagiza Maria mtawa aletwe ili ndoa ifungwe, binti akaletwa huku akionekana anang´ara kwa utukufu wa Mungu kama Malaika alipofikishwa hekaluni ndoa ikafungishwa na Kuhani Mkuu. Vifijo na nderemo vilisikika kutoka humo kwa watu wote waliohudhuria sherehe hiyo, watawa wenzake Maria wakampongeza na kumuaga, Makuhani na Mama walezi nao wakawapongeza wanaharusi hawa na kuwaaga, kwa kutoa Baraka zao. Siku watakatifu hawa walipofunga ndoa yao. Maria Bikira Mtakatifu alikuwa ametimiza umri wa miaka kumi na mine (14) kamili.

BAADA YA NDOA

Baada ya ndoa ya kufungwa Yoseph na Maria walikwenda kuishi kwa muda Yerusalemu kwenye nyumba yao ya chumba kimoja. Iliyokuwa imejengwa kwa mawe ndio nyumba aliyojenga na kuishi Yoseph kisha walihamia Nazareti katika nyumba waliokuwa wanaishi Joakimu na Anna. Bikira Maria ndiye aliyemshauri Mme wake kuhamia huko alifanya hivyo ili akarisishwe mali zote zilizoachwa na wazazi wake baada ya kufariki. Walipofika huko Maria alipewa urithi wa mali zote, naye akachukua sehemu ya mali hizo zingine akazigawa kwa ndugu zake, kwa masikini na kwa Mume wake.

MAISHA YA NDOA YAO

Kwa desturi ya mila zao Mvulana na Msichana wakifunga ndoa huwa mwiko kabisa kushiriki tendo la ndoa (Kujamiana), ingawa huruhusiwa nyumba moja desturi hii udumu kwa muda flani kadri ya maamuzi ya wazee wanaolinda sheria na mila wanavyoona inafaa na kuwapangia kipindi hiki huwaangaliwa kama wakati wa uchumba na kufahamiana tabia. Nao watakatifu hawa walizifahamu sheria na Mila zao, waliziheshimu na kuzifuata walielewa kwamba wakizikiuka watapaswa kushitakiwa kwa Kuhani na adhabu yake ilikuwa kupigwa mawe mpaka kufa. Hivyo waliogopa sana hukumu hiyo kwa hiyo walipokuwa bado katika kipindi hicho. Maria Mtakatifu alimweleza Yoseph kuwa alipendelea kuishi Maisha ya Ubikira na Utawa mpaka kufa, Yoseph aliposikia maneno hayo alifurahi sana naye akasema mpendwa wa moyo wangu tumshukuru Mungu kwa neema alizotujalia kwa kutukutanisha wenye nia moja, kwani hata mimi nilikwisha jitolea kwa Mungu kuwa Mtumishi wake tangu nikiwa na umri wa miaka kumi na miwili (12), basi nakuomba tuishi kama wachumba katika maisha yetu yote.

Bikira Maria aliposikia maneno hayo alifurahi sana, waliishi kitawa kila mmoja katika chumba chake cha kulala hasa waliohamia Nazareti, wakiheshimiana na kusaidiana kazi mbalimbali.

BIKIRA MARIA ANATOKEWA NA MALAIKA GABRIEL

Katika kipindi cha miezi sita na siku kumi na saba za kuishi baada ya ndoa yao, Maria Mtakatifu alitokewa na Malaika Gabriel alitumwa na Mungu aende kwenye mji uitwao Nazareti huko Galilaya kwa Msichana mmoja aitwae Maria, Mchumba wa mtu mmoja jina lake Yoseph wa ukoo wa Daudi, Malaika akaingia nyumbani mwake akamwambia "Salamu Maria, Umejaliwa neema nyingi, Bwana yu pamoja nawe" Maria aliposikia maneno hayo alifadhaika sana, akawaza maneno haya yana maana gani? Malaika akamwambia "Usiogope Maria kwa maana Mungu amekujalia neema, ni hivi; utapata mimba utazaa mtoto wa kiume na utampa jina Yesu".

Yeye atakuwa Mkuu na ataitwa Mwana wa yule aliye juu, Bwana Mungu atampa kiti cha Mfalme Daudi Babu yake. Kwa hiyo atautawala ukoo wa Yakobo milele na utawa wake hautakuwa na mwisho. Maria akajibu, yawezekanaje hayo, hali mimi ni Bikira? Malaika akamjibu "Roho Mtakatifu atakushukia na uwezo wake yeye aliye juu utakujia kama kivuli kwasababu hiyo Mtoto atakayezaliwa ataitwa Mtakatifu na Mwana wa Mungu. Ujue pia kwamba hata Elizabeth jamaa yako naye amepata mimba ingawa ni mzee na sasa ni mwezi wa sita kwake yeye ambaye watu walimfahamu kuwa tasa kwa maana hakuna lisilowezekana kwa Mungu." Maria akasema, "Mimi ni Mtumishi wa Bwana nitendewe kama ulivyosema". Kisha Malaika akaenda zake. Bikira Maria baada ya kusikia ujumbe huo wa Mungu hakumueleza Mmewe ikabaki siri yake. Alikumbuka alivyoelezwa na roho Mtakatifu akiwa bado yupo utawani, kuwa asimwambie mtu yeyote. Hivyo akayatunza maneno hayo yote moyoni mwake.

YOSEPH ANAGUNDUA MIMBA YA MARIA

Mimba ilipotimiza miezi mitano Yoseph ndipo alipogundua alishangaa sana kwa sababu alishindwa kujua ni jinsi gani Maria alivyoweza kuwa hivyo, kwani aliamini kuwa Maria alikuwa ni Binti mwenye tabia nzuri tena mwenye kulinda usafi war oho yake, alijiuliza uliza sana imekuaje! Kuna nini basi. Akajisikia uchungu Moyoni mwake akahofia hukumu ya kuuwawa kwa kupigwa mawe, kwa kuvunja sheria na mila za nchi yao.

Yote yakamsibu na kumfanya afikiri namna itakavyokuwa, atakapofikishwa mbele ya Kuhani na wazee wa mji hatimaye akapanga kutoroka lakini kabla ya kutimiza hadhima yake hiyo aliamua kumuomba Mungu amjulishe jinsi Maria alivyopata mimba hiyo akasema, "Mungu wangu, Mungu wa Ibrahim na Mungu wa Isacka kwani ninayo hakika binti huyu hakufanya mapenzi na mtu yeyote siku zote amezishika na kuzitimiza sheria za kitawa ila naamini kuna namna flani ya ukweli iliyotendeka" alisubiri Mungu amjibu ombi lake. Akaendelea kumtunza Maria kama kawaida naye Maria akawa Msichana mwenye upole sana, msikivu mwenye tabia nzuri ajabu asiye na wasiwasi wote usiokuwa na mawaa.

Mambo hayo Yoseph yalimshangaza sana.

Kwa kawaida mwanamke anayepata mimba nje ya ndoa huwa na wasiwasi mwingi lakini msichana huyu hata siku moja hakuonekana hivo……..

Mwisho.

 

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FAHAMU JINSI YA KUOMBA SALA YA VITA

MALAIKA MKUU MT. MICHAEL UTULINDE KATIKA VITA

SALA KWA AJILI YA KUFUNGULIWA KUTOKA KATIKA NGUVU ZA GIZA

CHANGAMOTO YA NDOTO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO

IBADA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

JINSI YA KUSALI ROSARI TAKATIFU YA BIKRA MARIA