IBADA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

 



IBADA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

 

SALA KABLA YA KOMUNIO – SALA YA KUUTULIZA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Yesu wangu, Mungu wangu na Bwana wa maisha yangu, sasa nataka kupokea komunio Takatifu, ili nikurudishie mapendo na kukufariji kwa ajili ya ubaridi wote na dhambi zote unazokosewa na watu katika Sakramenti hii ya mapendo. Ee Yesu, nakuomba unipe nguvu niishike na niishi nia hili. Nami najua ya kwamba wewe utakumbuka na kutimiza ahadi ya maneno uliyomwambia mtakatifu Margeth Maria Alacok, kwamba: “Utakuwa kimbilio langu katika maisha yangu na hasa saa ya kufa kwangu. AMINA”

Moyo wa Yesu matumaini yao wanaokufa katika neema yako – Utuhurumie.

Moyo wa Yesu malipo kwa dhambi zetu – utuhurumie.

AMINA.

 

 


1.   SALA YA KUMWOMBA ROHO MTAKATIFU AYAGEUZE MAISHA YETU.

 

Ee Roho Mtakatifu, upendo na uzuri, uchangamfu, wa Baba na Mwana, maua na harufu ya utakatifu wa Mungu. Moto Mtakatifu uliowashwa ndani yangu, uufanye moyo wangu uwe mpya, yasafishe madoa yote, ondoa giza, teketeza uchafu wote na uniumbie sura takatifu ya mwanao. Ewe Roho unayewaka na upendaye kukaa kwangu pekee ili uweze kunitakatifuza , washa moto huu wa mapendo, uingie moyoni mwangu na uingize na mwali wako wa moto. Ondoa mambo yote yenye nia mbaya na mipango mibaya. Nipe nguvu ya kuwa mtume awezaye kutekeleza kazi yako. Nipe neema ya kuwa mwali wa moto na uwake kwangu katika hali ya usafi wa moyo na upendo. Ee Mungu wangu, ninakusadiki kwa maana wewe ndiwe ukweli wenyewe. Ninakutumaini kwa maana wewe ni mwenye huruma isiyo na mwisho. Ninakupenda kwa Moyo wangu wote na zaidi ya vitu vyote, kwa sababu wewe ni Mkamilifu kabisa na nifundishe pia kumpenda na jirani yangu kama nafsi yangu kwa mapendo yako. Ninazijutia dhambi zangu zote kwa moyo wangu wote kwa sababu zimekuchukiza wewe uliye mwema sana. Kwa uthabiti nisikuchukize tena kwa neema yako.

 

AMINA

 

2. SALA YA KUUABUDU MOYO MTAKATIFU WA YESU KATIKA EKARISTI TAKATIFU

Kwa nguvu zangu zote za moyo wangu ninakuabudu. Ee Moyo Mtakatifu, na wa mwabudiwa sana, Moyo Mtakatifu wa Bwana wetu Yesu Kristu, mimi nataka kukupenda na kukusalimu kwa usikivu wote. Nipe neema yako ili nisikuudhi tena kwa sababu wewe ni mwema sana, Ee Moyo Mtakatifu sana, nisaidie kukupenda kwa moyo wangu wote, nisaidie kukupenda kuliko vitu vyote, nikupende kwa nguvu zangu zote na nikupende kwa uwezo wangu wote. Nisaidie nichukie kweli dhambi na uovu wote, ninatamani kuwa mali yako wewe uliyejitoa msalabani kwa ajili yangu kwa mateso makali.

Unionee huruma kwani mimi mdhaifu na usiniruhusu kupotea kamwe. Ninajitolea kabisa kwako ee Moyo wa mapendo kwa makusudi kwamba, utu wangu, maisha na mateso yangu yawe kwa ajili ya kukupenda, kukuheshimu na kukutukuza wewe sasa, siku zote hata milele. Ninakupenda ee moyo mwabudiwa wa Mwokozi wangu, ninaomba kwako uamuru moyo wangu na kila kitu ndani yangu kikutukuze sana na milele.

AMINA.

 

3. SALA YA KUJIANDIKA RAFIKI WA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Mimi…………………….. sitaki kujitumikia mimi mwenyewe bali ulimi wangu, macho yangu, masikio yangu, na mwili wangu mzima, uwe na kazi ya kuuheshimu kuupenda na kuusifu moyo Mtakatifu wako Ee Yesu Kristu. Ee Bwana Yesu, nakupa chochote kilicho changu. Yaani nafsi yangu, muda wangu, mali zangu, maisha yangu, mateso yangu, pamoja na masumbuko na mateso yote yatakayonipata katika maisha yangu. Leo, najifunga kwa sharti la kuwa rafiki yako mwaminifu na mwanao wa kweli, nikitenda matendo yangu yote kwa ajili ya kukupendeza wewe, nisaidie kukikataa katika maisha yangu chochote kitakachokuchukiza wewe.

Ee Moyo Mtakatifu, nakuelekea kwa kusudi moja tu, nalo ni upendo wangu kwako, uwe mlinzi wa roho yangu. Uwe mlinzi wa maisha yangu. Uwe hakika ya wokovu wangu. Uwe dawa ya udhaifu na unyonge wangu. Uwe mwenye kuponya vilema vyote vya maisha yangu. Na uwe makimbilio yangu salama, hasa saa ya kufa kwangu.

Ee Moyo mwema, saa ya kufa unioshe na kunitakasa kwa damu yako Takatifu ili nisiende kulaaniwa na Mungu Baba, Aliye na haki ya kunikasirikia. Ee Moyo wa upendo, mimi naweka tumaini langu lote kwako, kwa maana mimi naogopa kila kitu kwa ajili ya ubaya na udhaifu wangu, lakini natumaini kila kitu kwa upendo wako. Uniondolee basi kitu chochote kiwezacho kukuchukiza au kunizuia kuwa rafiki wa kweli na mwanao mwaminifu, maana mimi nataka heri yangu, furaha yangu na sifa yangu yote iwe katika kuishi na kufa kama rafiki yako mwaminifu na mwanao mpenzi.

AMINA.

 

4. LITANIA YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Bwana utuhurumie,    Bwana utuhurumie

Kristo utuhurumie,     Kritu utuhurumie

Bwana utuhurumie,    Bwana utuhurumie

Kristo utusikie,           Kristu utusikilize

 

 

 

Baba wa Mbinguni Mungu, Utuhurumie

(Kiitikio ni hicho kila baada ya Aya )

o   Mwana Mkombozi wa dunia Mungu

o   Roho Mtakatifu Mungu

o   Roho Mtakatifu Mungu mmoja

o   Moyo wa Yesu, Mwana wa Baba wa Milele

o   Moyo wa Yesu, uliotungwa na Roho

Mtakatifu mwilini mwa Mama Bikira

o   Moyo wa Yesu, ulioungana na Neno wa Mungu.

o   Moyo wa Yesu, ulio na utukufu pasipo mfano

o   Moyo wa Yesu, hekalu takatifu la Mungu

o   Moyo wa Yesu, hema la Yule aliye juu

o   Moyo wa Yesu, nyumba ya Mungu na mlango wa Mbingu

o   Moyo wa Yesu, tanuru yenye kuwaka mapendo.

o   Moyo wa Yesu, chombo cha haki na upendo

o   Moyo wa Yesu, unaojaa upendo na wema

o   Moyo wa Yesu, kilindi cha fadhila zote.

o   Moyo wa Yesu, unaostahili sifa zote

o   Moyo wa Yesu, unaotawala mioyo yote

o   Moyo wa Yesu, zinamokaa hazina za hekima na elimu

o   Moyo wa Yesu, mnamokuwa utimilifu wote wa Mungu

o   Moyo wa Yesu, uliopendelewa sana na Mungu Baba

o   Moyo wa Yesu, uliotuenezea maziada yake

o   Moyo wa Yesu, mtamaniwa wa vilima vya Milele

o   Moyo wa Yesu, wenye uvumilivu na huruma nyingi

o   Moyo wa Yesu, tajiri kwa wote wenye kukuomba

o   Moyo wa Yesu, chemchemi ya uzima na utakatifu

o   Moyo wa Yesu, malipo kwa dhambi zetu

o   Moyo wa Yesu, ulioshibishwa matusi

o   Moyo wa Yesu, uliovunjika kwa sababu ya ubaya wetu

o   Moyo wa Yesu, uliotii mpaka kufa

o   Moyo wa Yesu, uliochomwa kwa mkuki

o   Moyo wa Yesu, chemchemi ya faraja zote

o   Moyo wa Yesu, uzima na ufufuo wetu

o   Moyo wa Yesu, Amani na upatanisho wetu

o   Moyo wa Yesu, sadaka ya wakosefu

o   Moyo wa Yesu, unamokaa wokovu wao wenye kukutumainia

o   Moyo wa Yesu, matumaini yao wenye kuzimia kwako Moyo wa Yesu, sababu ya furaha kwa watakatifu wote

………………………………

Mwana kondoo wa Mungu, uondoaye dhambi

Za dunia                       Utusamehe Bwana,

Mwana kondoo wa Mungu, uondoaye dhambi

Za dunia                       Utusamehe Bwana,

Mwana kondoo wa Mungu, uondoaye dhambi

Za dunia                       Utusamehe Bwana,

 

K. Yesu Mwenye Moyo Mpole na Mnyenyekevu

W. Ufanye mioyo yetu ifanane na Moyo wako.

Tuombe: (W) Ee Mungu, Mwenyezi wa milele uuangalie Moyo wa Mwanao mpendelevu, pia na heshima na malipo aliyokutolea kwa ajili ya wenye dhambi, uridhike, uwaondolee wenye kuomba toba kwako kwa njia ya huyo mwanao Yesu Kristo, anayeishi na kutawala nawe pamoja na Roho Mtakatifu, Mungu daima na milele.

 

5. SALA YA MALIPIZI KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Yesu mpendelevu, unayewapenda mno watu, hata wasio na shukrani, wenye kuzembea na kukudharau. Tutazame sisi tunaojinyenyekesha chini ya Altare, tuna hamu ya kufanya malipizi kwa heshima ya pekee kwa ukatili wa wewe kupuuzwa na majeraha ambayo moyo wako Mpendelevu unatiwa na kuumizwa na watu popote

 

Ee Yesu, hata sisi tumehusika katika kushiriki kukuudhi na kukuletea uchungu mwingi. Kweli tunaujutia na kuusikitikia moyoni mwetu. Tunakiri makosa yetu na kukuomba kwa unyenyekevu msamaha, tukikujulisha kuwa tu tayari kufanya malipizi ya majuto na kitubio, bila ya kulazimishwa, siyo tu kwa ajili ya wale walio nje ya njia ya wokovu, wale wanaokataa kukufuata wewe Mchungaji na kiongozi wao, lakini pia kwa wale wasiojali maagano ya ubatizo wao, lakini pia kwa wale wasiojali maagano ya ubatizo wao, wakitupilia mbali nia njema ya amri yako wakishika mila na desturi za kiafrika zinazokataliwa na Injili, wanaoshika imani za kipagani, wanaoendekeza ushirikina, wanaoendekeza sadaka kwa mizimu, kupiga ramli na matambiko.

Sasa tuna kusudi la kutoa fidia na kufanya malipizi ya makosa kwa namna ya pekee, hasa zaidi kwa makosa haya:

1.    Ya kukosa heshima katika mioyo vitendo na vishawishi vingi vinavyofanywa duniani kwa kuwanasa na kuwadanganya watu wanyoofu.

2.    Kwa kutohudhuria Ibada za jumapili na siku zilizoamriwa.

3.    Kwa kufuru za kuchukiza wanazosema watu juu yako, juu ya Mama yetu Bikira Maria, na juu ya watakatifu wako.

4.    Kwa matusi juu ya Baba Mtakatifu na mapadri wako.

5.    Kwa uzembe na kufuru ambazo Sakramenti yako ya Ekaristi inatumiwa vibaya sana katika ulimwengu wa leo.

6.    Mwisho, kwa madhambi yote ya wanadamu ya kukataa na kupinga haki na mamlaka ya mafundisho ya kanisa lako uliloliweka.

Laiti kama ingaliwezekana kuosha kwa damu zetu maovu na machukizo ya aina hii. Na sasa katika ukaidi na ujeuri huo unaofanywa dhidi ya heshima yako ya kimungu tunapenda kutoa sadaka ile uliyotoa Msalabani kwa Baba yako na ambayo unaifanya tena kila siku katika Altare zetu. Tunapenda kuitoa tukiunganisha na malipizi ya Bikira Maria nay a watakatifu wote na ya waumini wote hapa duniani – wale wenye mapenzi mema.

Tunaahidi kweli, kulipa kadiri tunavyoweza kwa uzembe tunaoufanya kwa mapendo yako makuu kwa dhambi ambazo sisi na wengine tumezitenda zamani, kulipa kwa imani thabiti na maisha safi na kwa kutimiza amri ya mapendo nay a jirani, tunaahidi pia kuzuia wengine kadri tuwezavyo, wasikuchukize na pia kuwafanya watu wengine iwezekanavyo kukupenda na kukufuata.

Ee Yesu mpendelevu, kwa maombezi ya Bikira Maria aliye mfano katika kufanya malipizi, tafadhali pokea tendo letu hilo la hiari la malipizi na ukitupatia zawadi ya uvumilivu, tutakuwa waaminifu mpaka kufa katika wajibu wetu na utii kwako, ili sisi sote tuyafikie yale maskani yetu ya heri na furaha unapoishi wewe pamoja na Baba na Roho Mtakatifu mkitawala daima na milele.

AMINA.

 

 

 

 

7.   ROZALI YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

(Kwenye Msalaba)

Ee Yesu utupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu. Amina.

·         Baba yetu

·         Salamu Maria tatu

·         Atukuzwe baba

·         Nasadiki

(Kwenye kila tendo)

Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni kwa ajili ya dhambi ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo dhidi ya Sakramenti takatifu sana ya Altare, ninakutolea hapo kwa kuuridhisha pia, moyo wa Mama yako mpendevu Bikira Maria, na kwa mastahili ya watakatifu wote. Amina.

(Kwenye chembe za Salama Maria – zile 50)

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu uwakao mapendo wetu

-      Uwashe nyonyo zetu kwa upendo wako.

 

8.   NOVENA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

1.    Ee Yesu uliyesema “kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kukuomba neema ya ……………………

Baba yetu…………… Salama Maria …………………

Atukuzwe Baba…………

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wangu wote.

 

2.    Ee. Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu atawapeni”, tazama kwa jina lako ninakuomba neema ya………………..

Baba Yetu……………. Salamu Maria……………..

Atukuzwe Baba………

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wangu wote.

 

3.    Ee Yesu uliyesema “kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe” tazama, nikitiwa nguvu na ukweli wa maneno yako haya, ninakuomba

Neema ya …………………….

Baba Yetu…………………….. Salamu Maria ……………….

Atukuzwe Baba ……………..

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wangu wote.

 

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambao kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, yaani kutoacha kuwaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu na maskini na utujalie neema tulizokuomba kwa njia ya Moyo Imakulata wa Bikira Maria, Mama yako na mama yetu mpole.

Malizia kwa kusali:

“Salamu Malkia” na malizia: “Mt. Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee” x 3

 

4.   SALA YA MAOMBI

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu thabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wanazoziomba wengine. Wewe upo ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika kamwe, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja yetu.

 

Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda na kunipenda, kwani wewe Yesu upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu unihurumie, uyasikilize maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalohitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, sasa hata milele.

AMINA.

 

 

9.   SALA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU KUOMBA KUTIMIZIWA AHADI

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, Ututazame sisi tunaopiga magoti mbele yako ili kukuabudu, kukusifu, kukushukuru, kufanya malipizi kwa makosa ya zamani tukikumbuka ahadi ulizoahidi, tunathubutu kusema kwa matumaini yetu yote.

(K) Moyo Mtakatifu wa Yesu tujalie neema zote zilizo za lazima katika hali zetu za maisha.

 

Kiitikio: umeahidi Ee Bwana.

Moyo Mtakatifu wa Yesu tuletee amani nyumbani mwetu na katika jamaa zetu.

Kiitikio:……

Moyo Mtakatifu wa Yesu tufariji katika taabu, mateso na maisha yetu yote.

Kiitikio………..

Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwe Makimbilio yetu salama katika maisha hasa saa ya kufa kwetu.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu tushushie Baraka na neema nyingi katika kazi na shughuli zetu zote.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu fanya wakosefu wote wapate katika Moyo wako kisima na habari isiyo na mwisho ya huruma yako.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu fanya mioyo iliyo baridi, vuguvugu na legevu kuwa na bidii na hodari mwingi

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu fanya roho zilizo na bidii kuendelea kukamilika katika utakaso na utakatifu.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu bariki mahali panapowekwa kwa heshima sanamu ya Moyo wako katika nyumba zetu.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu wape mapadri na wale wanaoshughulikia wokovu wa roho za watu nguvu na uwezo wa kuigeuza hata mioyo migumu.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu andika na yasifutwe milele, majina ya wale wote wanaoanzisha, kueneza na kusali Ibada hii wao wenyewe na kwa watu wengine.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu tujalie kwa huruma ya moyo wako, sisi na wengine tutakaopokea komunio Takatifu Ijumaa ya kwanza ya mwezi kwa miezi tisa mfululizo neema ya kutubu tusife maadui wako wala kufa bila kupokea Sakramenti. Moyo wako uwe makimbilio yetu salama saa ile ya mwisho.

Kiitikio ……………

Moyo Mtakatifu wa Yesu fanya ufalme wako wenye nguvu utufikie ingawa shetani na jitihada za adui wako zinapinga vikali sana.

Kiitikio ……………

 

TUOMBE: Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, tunaweka matumaini yetu yote kwako. Ingawa mambo mengi yanatutisha sababu ya udhaifu wetu. Lakini bado tunatumaini mambo yote katika wema na huruma yako. Tunakusihi, uwe peke yako mapendo yetu yote, Mlinzi wa maisha yetu yote, nguvu katika udhaifu wetu wote na ukweli katika matendo na maneno yetu yote. Uwe shahidi wa wokovu wetu na makimbilio yetu wakati wa kufa kwetu. AMINA.

 

…………………………….

 

 


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FAHAMU JINSI YA KUOMBA SALA YA VITA

MALAIKA MKUU MT. MICHAEL UTULINDE KATIKA VITA

SALA KWA AJILI YA KUFUNGULIWA KUTOKA KATIKA NGUVU ZA GIZA

CHANGAMOTO YA NDOTO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO

JINSI YA KUSALI ROSARI TAKATIFU YA BIKRA MARIA