SALA KWA AJILI YA KUFUNGULIWA KUTOKA KATIKA NGUVU ZA GIZA


 SALA KWA AJILI YA KUFUNGULIWA KUTOKA KATIKA NGUVU ZA GIZA

Ifuatayo ni Sala nzuri sana kwajili ya mtu anayeshumbuliwa na nguvu za giza, Sala hii imeambatana na masharti au Muongozo tu awali ambao unakuwandaa vema kusali sala hii.

Na unapoanza kusali, Isali kwa kumaanisha na inapotokea unashindwa kusali wewe anayeweza aendelee kusali kwa niaba yako.

o   Upande wa maombi kumbuka kila siku kurudia maombi yako yale yale mpaka Mungu atakapo kujibu

o   Upande ya sehemu ya ahadi inayoambatana na maombi yako, kumbuka ahadi hizo unaingia wewe na Mungu wako, ikitokea umevunja ahadi zako kaungame haraka kwa Mungu wako.

o   Mwisho Sali Rozali ya huruma ya Mungu na ………

MASHERTI YA SALA HIZI

1.   Anza Sala hizi kwa kuungama kwanza dhambi zako zote tangu ulipokuwa na ufahamu, (ungama hata dhambi ambazo ulikuwa umeishaungama zamani)

2.   Baada ya hilo, omba misa maalumu, isomwe kwa nia yako. Usipokuwa na pesa basi itolee tu kimoyomoyo misa ambayo itakuwa ni kwa ajili ya kuanza rasmi kuzisali sala hizi. Wakati wa misa toa maombi maalumu  ya kuomba unachotaka na kuahidi kuwa ukipewa unachotaka utamtolea Mungu kitu gani (Ahadi hizi ni kama kuishi vizuri katika ndoa au kama mtu hana ndoa kuishi utakatifu wa kweli, yaani kuachana kabisa na dhambi kama ngono, kutupilia mbali maswala ya ushirikina, utoaji wa mimba kwa wanawake na yote ambayo dhamiri yako inaona ni machukizo kwa Mungu)

Ikumbukwe nguvu ya sala si katika maneno anayosali mtu bali ni matendo yake. Unapoomba neema maalumu kasha ukaishi ovyo ovyo kwa madhambi ni sawa na kumtukana Mungu. Matokeo si tu kuwa hutapata unachokiomba bali utasababisha pia hasira ya Mungu. Hata hivyo kwa tuko binadamu, si rahisi ukawa mtakatifu siku moja. Dhambi ndogo ndogo kama hasira, uvivu, kuwasengenya watu – hizi zitakuwepo. Lakini wakati wote wa sala hizi jikumbushe kuungama mara kwa mara, ili maisha yako yawe na Baraka ya kuweza kupokea unachokiomba.

 

3.   Pamoja sala hizi, kila siku Sali sala ya rozari ya kawaida ikiambatana na sala zilizoandikwa. Sala hizi siyo lazima zifuatane. Zinaweza kusaliwa kwa vipindi tofauti, La muhimu lazima zisaliwe zote kila siku. Rozari kuanza nayo, au kuisali baada ya sala hizi. Mwisho wa sala hizi imeandikwa Rozari ya Huruma ya Mungu. Hiyo ndiyo inahitimisha jumla ya sala hizi. Hizi ni sala ndefu lakini zenye nguvu ya uponyaji ajabu.

 

4.   Jitahidi kufunga walau mara moja kwa wiki muda wote unaposali sala hizi funga kwa kujinyima chochote utakachokimudu. Mfano, funga chakula, yaani ule mara moja kwa siku, au funga kuangalia televisheni, au siku hiyo Sali muda mrefu sana, na kadhalika. Kama una mashaka jinsi na namna gani ufunge kumuuliza padre yoyote akupe mwongozo. Hata hivyo kumbuka mafungo ya maana Zaidi ni kuacha dhambi. Hilo ni sharti muhimu sana kupata unachoomba

 

 

5.   Katika kipindi chote hiki uwe mtu mwadilifu kadiri ya uwezo wako wote. Epuka dhambi yoyote kubwa au ya makusudi. Kama ulishiriki chochote kwa kufahamu au kutofahamu kinachohusu mambo ya ushirikina, matambiko, au madawa yanayokatazwa na kanisa hakikisha unayaacha kwa roho yote kabisa, kabisa, kabisa. (Kanisa linakubali dawa asilia za kawaida tu. Endapo una mashaka kama dawa fulani inaruhusiwa au vipi basi, pata ushauri kutoka kwa padre)

 

6.   Ufahamu kuwa unaposali sala hizi siku za mwanzo kitakuwa ni kipindi cha majaribu mengi. Maana yake ni kwamba shetani anataka kukukatisha tamaa. Yashinde yote kwa nguvu ya sala, na Imani. Utakapokuwa unaendelea, magumu yataanza kupungua. Magumu haya ninayosema ni kwa mfano: Unaweza kujikuta una hasira sana, au una usingizi wa ajabu, au kuugua ugua, wengine wanaposali sala hizi huwa hadi wanatapika, wengine tumbo linawauma sana, ndoto za ovyo na kadhalika. Haya yote ukikazana na kuzama zaidi na Zaidi yataisha.

 

7.   Sali sala hizi kwa mfululizo kila siku hadi Mungu atakaposikiliza ombi lako. Usihesabu umesali wiki ngapi au miezi mingapi. Jambo muhimu ni kuwa usizisali kama unasoma gazeti. Zama kwa moyo wako wote na kwa Imani yako yote kabisa. Ukijua wazi kuwa uko mbele ya Mungu na kuwa unapambana na shetani. Iweke nafsi yako yote kwa unyenyekevu wako wote mbele ya Mungu. Siri ya uponyaji iko hapo. Na usiwe na mashaka yoyote kabisa.

 

8.   Ukiweza kila unapopata uwezo omba misa kwani sala ya misa ndiyo sala kubwa kuliko zote. Omba misa mara nyingi kadri utakavyoweza. Na hata usipoiomba misa, katika kipindi chote kila uingiapo kanisani, ombi lako liwe hilo hilo la nia uliyoweka. Hukatazwi pia kuongeza nia zingine, lakini nia kubwa iwe hii. ……………………………….

 

SALA KWA AJILI YA KUFUNGULIWA KUTOKA KATIKA NGUVU ZA GIZA

1.   KWA JINA LA YESU

Katika Jina la Yesu wa Nazareti, Baba wa Mbinguni, ninakuinulia mkono wangu wa kuume. Mimi mwanao, ……. ( hapa taja jina lako)

Nitazame Bwana maana nguvu na uwezo wote unatoka kwenye kiti chako cha enzi. Kama ilivyoandikwa katika zaburi ya 62:11-12 "Mara moja amenena Mungu, mara mbili nimeyasikia haya, ya kwamba nguvu zina Mungu. Na fadhili ziko kwako ee Bwana, maana ndiwe umlipaye mtu sawa sawa na haki yake "

 

Baba wa Minguni, ninapokea nguvu kutoka kwako sasa kwa jina la Yesu. Ninatumia nguvu hizi kufuta, kuvunja, kuharibu na kujitenga mwenyewe kutoka kwenye laana zote za maagano yaliyofanywa dhidi yangu. Ninaamuru laana zote pamoja na mapatano na mazindiko yaliyojificha popote dhidi maisha yangu kujidhihirisha sasa katika jina la Yesu. Ninaamuru moto wa Roho Mtakatifu na damu ya Yesu kuwadhihirisha wote. Ninaziharibu nguvu zenu zote kwa jina la Yesu – AMINA.

Baba yetu uliye Mbinguni x 10. Salamu Maria x 10, KISHA Atukuzwe Baba x 3.

 

2.  DHAMBI NA LAANA ZA WAHENGA WANGU.

Katika jina lenye nguvu na uwezo la Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti, ninatubu dhambi zilizofanywa na wahenga wangu. Laana ya hizo dhambi zinaniandama hadi leo mimi. Ninavunja na kuharibu laana zote, maagano na matambiko kutoka kwa mababu zangu, hata kama laana hizo zimesababishwa na uovu wowote walioufanya. Ninaziharibu kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti – AMINA.

 

Naziharibu na kuzivunja laana zote, mapatano na matambiko katika upande wa Baba yangu na Mama yangu katika Jina la Yesu. Bila kujali ni haina gani ya laana iliyowekwa juu yangu. Bila kujali ni maagano gani wahenga wangu wamefanya na shetani, na bila kujali ni wapi wamefanya mambo ya matambiko na mazindiko juu yangu: iwe ni angani, duniani au baharini. Ninayaharibu yote kwa jina la Yesu – AMINA.

Pia ninavunja laana, maagano na matambiko niliyofanyiwa na Baba yangu, Mama yangu na wazazi wao (Babu na Bibi) kutoka kizazi chochote kwa upande wa Baba yangu na Mama yangu bila kujali laana, matambiko, mazindiko, mapatano na ushirikiano wao wote kuwa yalifanyika wapi. Ninaamuru yote kuvunjika na kuharibiwa katika jina la Yesu Kristo – AMINA.

Baba Yetu Uliye Mbinguni x 10. Salamu Maria x 10, KISHA Atukuzwe Baba x 3

 

3.  KUTOKA KWANGU MWENYEWE

Katika Jina la Yesu ninakwenda kinyume na laana zote nilizozisababisha mimi mwenyewe juu ya maendeleo yangu ya maisha yangu kwa kujua au kutojua.

Ninakuvunja wewe laana popote pale ulipojificha. Iwe angani, duniani au baharini. Ninaharibu na kuzivunja nguvu zako zote katika Jina la Yesu. Ninakuja kinyume na maagano niliyoyafanya na miungu na pepo wachafu, maruhani, majini, majini bahari, waume wa kipepo, wanawake wa kipepo, watoto wa kipepo na mizimu. Iwe katika ulimwengu huu au ulimwengu wa kiroho au hata katika ndoto.

Ninavunja maagano yote katika jina la Yesu. Mazindiko yote niliyojifanyia nayo ninaharibu yote. Ninajiondoa katika mazindiko hayo. Ninalifuta jina langu kutoka katika kitabu cha shetani. Ninajitangazia uhuru leo katika jina la Yesu. Ninajifunika kwa damu ya Yesu kristo wa Nazareti – AMINA.

Baba Yetu uliye Mbinguni x 10. Salamu Maria x 10, KISHA Atukuzwe Baba x 3.

 

4.  KWA KUTOMTII MUNGU

Ninaziungama na kuzitubu dhambi zangu kwa jina lako Baba. Katika jina la Yesu ziondoe laana zote juu yangu kwa ajili ya kutozitii amri zako. Umkemee yule aliye katika maisha yangu, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Malaki 3:8-12 "Ondoa zinge, tunutu na viwavi kutoka kwangu" Ninyeshee mvua za mwanzo na za mwisho. Nijaze tena Baraka zako, katika jina la Yesu – AMINA.

Baba Yetu uliye Mbinguni x 10. Salamu Maria x 10, KISHA Atukuzwe Baba x 3.

 

5.  KUJITENGA NA ULIMWENGU

Baba wa mbingu, ninajishusha na kujitenga na Ulimwengu na vishawishi vyake na laana zake zote. Najitenga tena na maagano na mazindiko yote niliyofanyiwa na niliyoyafanya, kwa kufahamu au kwa kutofahamu. Mimi niko huru sasa. Na kwa tamko la kinywa change sasa, namchagua Bwana wangu Yesu kristu tangu leo kuwa Bwana na Mfalme wangu. Tangu sasa mimi ni kiumbe kipya. Roho Mtakatifu yu juu yangu sasa. Na tangu sasa nayaweza yote katika jina la Yesu Kristo anitiaye nguvu. Ninamwaibisha shetani sasa na ninamtangazia uhuru wangu katika jina la Yesu Bwana wangu. Ninaharibu mipango yote ya shetani aliyo nayo juu ya maisha yangu. Popote anapojificha, ninaamuru moto wa Roho Mtakatifu umuunguze usiku na mchana hata milele kwa jina la Yesu – AMINA

Baba Yetu Uliye Mbinguni x 10. Salamu Maria x 10, KISHA Atukuzwe Baba x 3.

 

6.  KUJIFUNIKA KWA DAMU YA YESU

Najifunika sasa kwa damu ya Kristo, ninajilowesha mimi mwenyewe. Ninaifunika nyumba na chumba ninamoishi, Nawafunika majirani zangu wabaya, naifunika kazi yangu, naifunika mipango yangu yote na nakifunika kila nilicho nacho. AMINA

Damu ya Kristo – Nioshe,

Damu ya Kristo – Nitie nguvu,

Damu ya Kristo – Niburudishe,

Damu ya Kristo – Uwe juu yangu,

Damu ya Kristo – Uwe chini yangu,

Damu ya Kristo – Uwe nyuma yangu,

Damu ya Kristo – Uwe mbele yangu,

Damu ya Kristo – Uwe ndani yangu,

Damu ya Kristo – Unikinge

Damu ya Kristo – Unipiganie,

Damu ya Kristo – Uniimarishe dhidi ya mwovu,

Damu ya Kristo – Unilinde dhidi ya vishawishi

AMINA.


UNAWEZA PIA KUTAZAMA VIDEO HII KWA AJILI YA KUJIFUNZA ZAIDI  




7.  KUOMBA NEEMA MAALUMU

1.   Yesu wangu, wewe ulituahidi kwamba: `Ukweli nawaambia, ombeni mtapewa, tafuteni mtaona, na bisheni hodi mtafunguliwa, `Nami kwa Imani kubwa nabisha hodi, natafuta na naomba neema ya …….. (taja ombi lako)

Baba Yetu………………………. Salaamu Maria ……………. Atukuzwe Moyo Mtakatifu wa Yesu, Nakuamini na najiaminisha kwako.

 

2.   Yesu wangu, uliyesema:- "Ukweli nawaambieni, chochote muombacho kwa Baba yangu kwa jina langu, Yeye atawapeni," Nami, kwa kutaja jina lako Takatifu, naomba neema ya …………… (Rudia ombi ulilotaja juu)

Baba yetu ……………………………. Salaamu Maria …………….. Atukuzwe Baba Moyo Mtakatifu wa Yesu, Nakuamini na najiaminisha kwako.

 

3.   Yesu wangu uliyesema, :- " Mbingu na dunia zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe," Nami nikijiaminisha kwa ahadi ya maneno hayo matakatifu naomba neema ya …….. (Rudia mara ya tatu ombi ulilotaja)

 

Baba yetu …………………………

Salamu Maria …………………….

Atukuzwe Baba …………………..

Moyo Mtakatifu wa Yesu, Nakuamini na najiaminisha kwako.

 

4.   Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambao kamwe hauwezi kuacha kutuhurumia sisi wakosefu, tuhurumie wanao wakosefu, na tujalie neema tulizokuomba kupitia kwa Moyo safi wa Bikira Maria, ambaye ni mama yako na Mama yetu pia.

Ee Mtakatifu Yosefu , Baba Mlishi wa Familia Takatifu Utuombee..

(Rudia mara tatu maneno hayo)

 

8.  AHADI

Ili kupata neema hii ya …………………. Na pia iambatane na kufunguliwa Baraka zote kutoka mbinguni, name nakuahidi Mungu wangu kuwa na mwenendo mwema kweli wa Kikristo. Kubeba msalaba wangu kama anavyoniagiza Yesu na kuishi kwa kuangalia mbingu kila siku. Najiweka mimi mwenyewe chini ya usimamizi wa Mama Bikira Maria mama mwenye usafi kamili wa moyo na mama yangu tangu sasa nikimwahidi kuishi maisha safi ya Kikristo, kwa unyenyekevu kasha, nakukabidhi maisha yangu yote. Nakuahidi (1) kutunza usafi wa moyo (2) kutojihusisha na nguvu za giza hadi kufa (3) kudumu katika sala. Naomba tangu sasa maisha yangu yote yafunikwe tena na damu ya Yesu yenye Baraka na nguvu isiyoshindwa sasa hadi saa ya kufa kwangu – AMINA

 

9.  LITANIA YA HURUMA YA MUNGU

Bwana utuhurumie ……………………….

Kristu utuhurumie …………………………

Bwana atuhurumie ……………………….

Kristu utusikie ………………… Kristu utusikilize

Baba wa mbinguni Mungu….. Utuhurumie

Roho Mtakatifu Mungu ……….. Utuhurumie

Utatu Mtakatifu Mungu mmoja ………….. Utuhurumie

 

v Huruma ya Mungu iliyo sifa kuu ya Muumba wetu ……………….

 

TUNAKUTUMAINIA

v Huruma ya Mungu iliyo kilele cha Ukamilifu wa mwokozi wetu,

v Huruma ya Mungu iliyo upendo usiopimika wa Roho Mtakatifu.

v Huruma ya Mungu iliyo fumbo kuu la utatu Mtakatifu.

v Huruma ya Mungu iliyo ishara ya uwezo Mkuu wa Mungu Mwenyezi,

v Huruma ya Mungu iliyoonyeshwa katika kuziumba Roho za Malaika,

v Huruma ya Mungu iliyotuumba na kutufanya tuwepo,

v Huruma ya Mungu inayoushika na kuuhuisha ulimwengu mzima,

v Huruma ya Mungu inayotujalia maisha ya kutokufa,

v Huruma ya Mungu inayotukinga na adhabu tunazostahili,

v Huruma ya Mungu inayotufanya wenye haki, katika neno aliyejifanya mtu.

v Huruma ya Mungu inayofurika kutoka katika Majeraha ya Kristo,

v Huruma ya Mungu inayobubujika kutoka ndani ya Moyo Mtakatifu wa Yesu,

v Huruma ya Mungu aliyotupatia Bikra Maria Mtukufu kabisa awe kwetu "Mama wa Huruma"

v Huruma ya Mungu inayoonyeshwa katika ufunuo wa Mafumbo Matakatifu ya Mungu,

v Huruma ya Mungu ilionyeshwa katika kuanzisha kanisa Katoliki

v Huruma ya Mungu inayopatikana katika mafumbo ya Sakramenti Takatifu.

v Huruma ya Mungu inayotolewa kwa wanadamu wote kwa njia ya ubatizo na kitubio,

v Huruma ya Mungu inayotolewa katika Sakrameti ya Ekaristi na daraja takatifu,

v Huruma ya Mungu inayoonekana katika uongofu wa wakosefu,

v Huruma ya Mungu inayoonyeshwa katika kuwatakatifuza watu wenye haki,

v Huruma ya Mungu chemchem ya afya kwa wagonjwa na wote wanaoteswa,

v Huruma ya Mungu iliyo faraja ya wote wenye uchungu moyoni,

v Huruma ya Mungu iliyo tumaini la roho zinazokata tamaa,

v Huruma ya Mungu iliyo mwenzi wa daima na popote wa watu wote.

v Huruma ya Mungu inayotuletea neema zote.

v Huruma ya Mungu iliyo Amani yao wanaokufa.

v Huruma ya Mungu iliyo tumaini na faraja ya marehemu Toharani.

v Huruma ya Mungu iliyo furaha ya Mbinguni kwa watakatifu wote,

v Huruma ya Mungu iliyo taji la watakatifu wote,

v Huruma ya Mungu chemchemi ya miujiza ya daima.

Mwanakondoo wa Mungu, uliyetuonyesha huruma yako kuu katika kuikomboa dunia kwa msalaba wako Mtakatifu,

W. UTUSAMEHE BWANA.

Mwanakondoo wa Mungu, anayejitolea kwetu kwa mapendo na Huruma katika kila adhimisho la sadaka ya misa Takatifu,

W. UTUSAMEHE BWANA.

Mwanakondoo wa Mungu unayeondoa dhambi za dunia kwa njia ya huruma yako isiyo na mwisho.

W. UTUHURUMIE

Bwana utuhurumie……. Bwana utuhurumie

Kristu utuhurumie……. Kristu utuhurumie

Bwana utuhurumie….. Bwana utuhurumie.

………………………..

Ee Damu na Maji, yaliyobubujika kutoka katika Moyo wa Yesu kama chemchemi ya huruma kwetu…… TUNAKUTUMAINIA

………………………..

Tuombe

Ee Mungu uliye na huruma isiyo na mwisho, na hazina za wema na upendo wako hazina mipaka, tunakusihi, ututazame sisi watu wako huku duniani na kutuongezea huruma yako tena na tena, ili itusaidie, tusije tukakata tamaa hata mara moja, hata tunapokumbana na majaribu makubwa kiasi gani, bali tuweze daima kuzielekea na kuzishika amri zako kwa Imani, matumaini, na mapendo na kutimiza daima mapenzi yako Matakatifu, ambayo ndiyo Huruma Yenyewe.

 

Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristu Mwanao, Mfalme wa Amani na Huruma, aishiye na kutawala Nawe na Roho Mtakatifu, kwa pamoja mkituonyesha Huruma isiyo na mwisho, daima na milele.

Amina.

TAZAMA VIDEO HII KUJIFUNZA ZAIDI





Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FAHAMU JINSI YA KUOMBA SALA YA VITA

MALAIKA MKUU MT. MICHAEL UTULINDE KATIKA VITA

CHANGAMOTO YA NDOTO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO

IBADA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

JINSI YA KUSALI ROSARI TAKATIFU YA BIKRA MARIA