NGUVU YA SALA ALIZOFUNDISHWA MTOTO GRACE


NGUVU YA SALA ALIZOFUNDISHWA MTOTO GRACE                                          


(UMRI WA MTOTO NI MIAKA 12) MNAMO MWAKA 2015 NA MALAIKA MICHAEL

 

UTANGULIZI

Sala hizi ni sala zilizoandikwa na mtoto Grace mwenyewe, akiongozwa na Mt. Michael Malaika Mkuu, na sala hizi ziliandikwa baada ya ombi maalum toka kwangu, hii ni baada ya kutaka kudadisi Malaika wanamfundisha nini mtoto Grace awapo usingizini, maana wakati mwingine mtoto Grace akiwa kalala na ukienda kumwamsha kama nafsi yake haipo hapo, alinyoosha mkono tu kutoa ishara ya kusubiri, basi tuliweza kusubiri mpaka alipozindika peke yake.

 

Hata pale alipoweza kuamka ulipomuuliza alikuwa wapi, naye alijibu wakati umekuja kuniamsha, Mt. Michael Malaika Mkuu alikuwa ananifundisha sala, au anaweza kukujulisha alikuwa na Malaika Enjo au Anjelina hawa ni Malaka waliojitambulisha kwa Majina hayo ndani ya familia, basi baada ya kugundua kuna kitu kinaendelea, ndipo nilipomwomba mtoto Grace aweze kuandika sala zote anazofundishwa na Malaika.

 

Mt. Malaika Michael siku moja alikuja na kuongea nami na kusema, mtoto Grace ataweza kuandika sala baadhi tu, msimlazimishe kuandika sala zote maana kuna sala zingine zina nguvu sana na endapo ataziandika nyinyi binadamu mnaweza kuzisali kawaida bila kujiandaa na kutokujua nguvu ya matokeo ya sala hizo, hivyo sitatoa kibali cha uandishi wa sala hizo ambazo zitabaki kuwa ni sala za mtoto Grace ambazo anaweza kuzitumia yeye tu katika ulimwengu wa roho.

 

Baada ya maelezo hayo sikuwa na namna yeyote zaidi ya kuwa mtii, ndipo nilipoambulia sala hizi ambazo leo nakushirikisha nawe, kuzisali, sali kwa imani na kumaanisha hakika utaona huruma ya Mungu na Upendo wake wa ajabu juu yetu sisi wanadamu. Karibu tusali pamoja Amina.

 

Shukrani

Napenda kutoa shukrani za dhati kwa Mwenyezi Mungu muumba mbingu na nchi kunitia nguvu kuweza kutengeneza kitabu hiki kidogo cha sala.

Natoa shukrani kwa mtoto Grace katika uandishi wa sala hizi.

 

Na kwa umuhimu nimshukuru Mt. Michael Malaika Mkuu kuwa pamoja nasi kwa ukaribu wa pekee, na kushiriki kwa namna ya pekee kumfundisha mtoto Grace sala nyingi za vita vya kiroho na kuifanya familia kuwa na Amani na leo kufanikisha kitabu hiki kidogo cha sala ambapo ni kati ya mfululizo wa vitabu vinavyomgusa mtoto Grace ikiwa ni toleo la tatu.

 

Nawashukuru ndugu zangu, ambao wamekuwa wafadhili wakubwa wa familia yangu, pia namshukuru mke wangu ambaye amekuwa kiongozi bora wa Imani ndani ya familia.

 

Mwisho nikushukuru wewe msomaji ambaye umeguswa na kitabu hiki, Mungu Mwenyezi Muumba mbingu na nchi azidi kukutia nguvu katika maisha safi ya kiroho Amina.

 

 

1.    SALA YA KUVUNJA MADHABAHU ZA KICHAWI

Mungu Baba Mwenyezi uliyeumba mbingu na dunia tunakushukuru kwa kutuweka duniani na kutupatia nguvu, Ee Mungu tunaomba utupe nguvu za kukutumikia wewe, sisi tumekosa sana tunaomba msamaha kwa dhambi zetu, Ee Mwenyezi Mungu kuna binadamu wanaojenga madhabahu kinyume kabisa na mapenzi yako, tunaomba nguvu sasa na tunakwenda kinyume na madhabahu za kichawi popote pale zilipo iwe kwenye bahari ninaziteketeza kwa jina la Yesu Kristu wa Nazarethi, roho Mtakatifu tunaomba ututangulie kwa jina la Yesu Kristu, Mungu Baba Mwenyezi tunaomba utupe nguvu za kubomoa nguvu za kichawi, popote zilipo, na madhabahu zake zote tunaomba nguvu ya afya ya roho na mwili – Amina.

 

2.    SALA YA KUVUNJA VIOO (SCREEN) NA MAPEPO YANAYOZUIA MAOMBI

Ee Mungu tunakwenda kinyume dhidi ya mapepo yote yanayozuia maombi, tunakwenda kinyume dhidi ya screen za kipepo, za kichawi za majini zinazotumika kuangalia watu wa Mungu, tunapofua macho yenu ninyi mapepo mnaoshika maombi ya watu wa Mungu, tunakatakata mabawa yenu kuanzia sasa na kila pepo arukaye, kila pepo ashirikiaye maombi, Ee Mungu tunaomba umtume Malaika Michael akawateketeze kwa upanga wako Mtakatifu, tunaomba utujalie nguvu shetani asipate nafasi juu yetu, juu ya watu wote wa Mungu Amina.

-      Mtakatifu Michael Malaika Mkuu- utulinde na kutuokoa. Amina

 

3.    SALA YA KUOMBEA WATOTO WANAOTOLEWA MIMBA

Ee Mungu tunakushukuru kwa afya njema, tunaomba Mungu kwa msaada wako na kwa nguvu zako za ajabu uliumba watoto na ukasema watoto wadogo wote waje kwako, ila kwa kuwa sisi binadamu hatukutii, sisi tumefanya isivyo kabisa.

Ee Mungu tunaomba msamaha kwa ajili ya hili tatizo la utoaji mimba, Ee Mungu tazama dunia ya sasa inapoelekea sio kuzuri, tunaomba msaada wa maombezi ya mama Bikra Maria, mama yetu, mama wa Kanisa, mama wa watoto yatima, mama wa watoto wanaotolewa mimba.

            Tunajua hili ni chukizo mbele za Mungu na kwa mama yetu Bikra Maria, tunaomba kwa uwezo wako Mungu uwashushie huruma wakina mama, mabinti wa sasa na kizazi kipya hata kijacho huruma yako, wajue kwamba utoaji wa mimba haukupendezi wewe Mungu wetu unakuchukiza, pia waonee huruma kwa viumbe hivyo wanavyohitaji kivikatiza maisha, kuvihukumu bila makosa kwa maana watoto hao ni watoto wa Mwenyezi Mungu hawana makosa.

            Ee Mungu wape watu wote wanaohitaji kutoa mimba huruma na wajue ya kwamba watoto hao pia wanahitaji kuishi kama wenyewe wanavyoishi na pia wakuogope wewe Mungu uliye waumba na kuwapatia uhai, tunajua sisi wanadamu hatuna mamlaka ya kutoa uhai wa mtu mwingine isipokuwa wewe tu, hivyo basi tunaomba msaada wako, uwajalie binadamu huruma na wajue hawana mamlaka ya kutoa uhai wa mtu mwingine. Tunaomba hayo yote kwa njia ya Kristu – Amina.S

Bikra Maria mama wa watoto x 3 tuombee

Bikra Maria mama wa msaada wa dunia utuombee x 3

Salamu Maria x 3     

 

4.    SALA YA KUOMBA ULINZI WA MALAIKA

Ee Mungu Mwenyezi uliyeumba binadamu na Malaika tunakushukuru kwa kuweza kuumba vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana, kwa nguvu na uwezo wako wa ajabu ulimuumba binadamu na kila binadamu ulimpatia Malaika walinzi na sisi pia hatunabudi kuwaheshimu, tunaomba uwatume Malaika wako waje watulinde katika hatari zote za roho na za mwili, tunaomba Malaika wako watulinde, watuongoze sehemu ya kupita siku zote za maisha yetu, tunaomba enyi Malaika ulinzi wenu uwe pamoja nasi, msituache katika matope, mtufundishe jinsi ya kusali, jinsi ya kumheshimu Mungu wetu Amina.

-      Enyi Malaika wetu Watakatifu - mtuombee x 3

-      Enye Malaika walinzi wetu – mtuombee x3

 

5.    SALA YA KUOMBEA FAMILIA

Ee Mungu Baba Mwenyezi, tunakushukuru kwa kuweka familia, ukaweka baba, mama na watoto na pia ukamfanya baba kuwa kichwa cha familia na ukampa mamlaka ya kuongoza familia, tunaomba huruma yako ishuke katika familia zetu, weka amani katika familia, weka upendo, furaha na kuweza kuheshimiana sisi wenyewe kwa wenyewe, mpe nguvu baba wa familia, ondoa nguvu yoyote inayomfanya kutokujua wajibu wake kama baba wa familia, pia wabariki watoto uwajalie heshima kwa wazazi wao, unyenyekevu kwa wazazi wao, Ee Mwenyezi Mungu tunaomba ulete amani kwenye familia zenye mfarakano, familia zisizokuwa na amani, upendo, furaha, familia zenye vurugu ukarudishe amani, upendo Amina.

Mama wa familia Takatifu utuombee x 3

 

6.    SALA YA KUOMBEA MAPADRI NA WATAWA

Ee Mungu baba Mwenyezi tunakushukuru kwa afya ya roho nay a mwili, pia tunashukuru kwa ajili ya kulipatia Kanisa lako Mapadri na Watawa. Mapadri hao wanayo nguvu ya kugeuza mwili na damu ya Bwana wetu Yesu Kristu, Mapadri hao wanao wajibu mkubwa wa roho zetu, Ee Mungu tunaomba ulipatie Kanisa lako Mapadri walio watakatifu wa kulitumikia Kanisa lako takatifu na pia tunaomba uwajalie Mapadri na Watawa moyo wa uvumilivu, wakutangaze wewe na kukuheshimu, tunaomba uwajaliye moyo wa unyenyekevu, amani, upendo, furaha, uwajalie waweze kushinda hila zote za shetani, wape nguvu ya kulitangaza neno lako pasipo woga wowote na mwisho waweza kushinda hila za yule mwovu, kwa maombezi ya Bikra Maria Rosa mystica aweza kuwaombea Mapadri na Watawa wote. Awape moyo wa kuvumilia majaribu yote watakayokumbana nayo. Amina.

 

Ee Mungu mwenye huruma twakuomba uwajaze nguvu mioyo yao, isiweze kuwa baridi na pia waweza kutimiza ahadi waliyoiweka kwako katika madhabahu yako mpaka kufa kwao, waweze kuishi maisha ya usafi wa moyo – Amina.

Maria Rosa mystica utuombee x 3

Wote, waweza kuishi maisha ya kumpendeza Mungu utuombee x 3

Baba yetu x 3, salamu maria x 3, atukuzwe x

 

 

7.    SALA YA KUOMBEA MATAIFA

Ee Mwenyezi Mungu Muumba Mbingu na dunia kwa uwezo wako wa ajabu, uliumba binadamu wakujue wewe, wakutumikie wewe, lakini hawafanyi hivyo, tunaomba ushushe mkono wako wa Baraka katika Mataifa yote, leta amani, upendo na furaha katika Mataifa yote tunakuomba ukayabadirishe Mataifa yanayomwaga damu, hayana amani wala furaha na uyaletee amani na furaha ili kusudi mwovu asipate nafasi katika Mataifa hayo, Mungu Mwenyezi tunajua kwamba wewe pekee ndiye uliyetupatia uhai, wala si mwingine na wewe ndio mwenye uwezo wa kutoa uhai wa mtu.

 

Tunaomba kwa maombezi ya Bikra mama wa msaada, mama wa neema zote tunaomba uyalinde Mataifa yote uzuie vita na pia ulete amani katika Mataifa yote, tunajua ya kwamba pasipo neema ya Mungu hatuwezi chochote hivyo basi tunaomba amani kwa Mataifa yote yenye kukuabudu, yenye kukuheshimu na hata yenye kukudharau,na yenye kukufuru wewe Mungu, tunaomba hasira yako isitushukie sisi wanao japo tunajua tumekukosea wewe, tunaomba msamaha kwa yote tuliyo yafanya ambayo hayakupendezi wewe, pia tunaomba msaada wa Bikra Maria mama yetu, mama wa Mataifa, mama wa watoto wote, Ee Mungu tunaomba huruma yako itukinge na hila zote za yule mwovu shetani na mwovu asipate nafasi ya kutudhuru.

 

Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristu wa Nazareti – Amina

Bikra Maria msaada wa daima utuombee x 3

Bikra Maria wa neema utuombee x 3

Salamu maria x 3

 

8.    SALA YA KUMFUNGA ADUI YEYOTE ANAYEINGILIA MAISHA YAKO

Ninamfunga mwovu anayenisumbua katika maisha yangu na ukoo wangu, ninamfunga na mamlaka yake, ufahamu wake wa kichawi, vitu anavyotumia visipate kurudi tena na mwisho akaombe msamaha, katika jina la Yesu Kristo naomba.Amina

 

9.    SALA YA KUJIKINGA  NA MUOVU

Ewe Roho Mtakatifu tunaomba utukinga na muovu yoyote, akija akutane na damu ya Yesu, nayo imemchome atakaporudi damu hii ikaendelee kumchoma mpaka kwenye kiti anachokaa na vitu vyake na washiriki wake wakateketee wote. Amina.

 

10. SALA YA KUVUNJA LAANA ZA UCHAWI (03/07/2015)

Anza na kusali sala ya Mt. Michael, ninawafunga na kuvunja nguvu zenu wachawi wote na sorcerer wote wanaofuatilia maisha yangu kwa namna yeyote ile.

Kwa nguvu ya kusulubiwa na damu ya Yesu Kristo iliyomwagika msalabani, ninasambaratisha njia zote za kipepo (sprit-guides) wa wachawi na waabudu mizimu, Roho za wahenga zilizofutilia maisha yangu kwa njia ya nguvu zao za kichawi ili kuweza kunidhulu, kwa jina la Yesu ninawasambaratisha. Amina.

 

 

11. JIWEKE HURU NA MAAMBUKIZO YA KICHAWI

-       Sali kwanza sala ya Mt. Michael (inayojulikana)

-       Mungu baba nakushukuru kwa damu ya Yesu Kristo mwano mpendwa, leo nakuja kwako kwa neema yako uniweke huru kutokana na kile ambacho nimeambukizwa mwilini kwa njia ya Roho.

 

Nasalimisha kila mbegu ya kichawi iliyopandwa ndani yangu naomba damu ya mwanakondoo inisafishe, pia kila ambukizo lolote ambalo limeitishwa ndani yangu wakati ningali tumboni mwa mama yangu, nalisambaratisha ambukizo hilo kwa jina la Yesu na lisipate nafasi tena kwangu kwa jina la Yesu. Amina.

 

12. MAOMBI YA VITA DHIDI YA MAADUI WANAOJIFICHA KWENYE MWAMVULI WA MASWALA YA MUNGU.

(Wale wanaovaa mavazi ya kondoo hali ndani ni fisi) 04/08/2015

Kwa maombezi ya Bikra Maria Mtakatifu na watakatifu, Ee Mungu baba ninaomba utume Roho Mtakatifu aweze kumfichua mchana kweupe shetani yule ambaye amejificha kwenye mwamvuli wa dini hali ndani ni fisi, kwa jina la Yesu ninamfunga ili asipate kurudi tena. Amina

 

13. SALA DHIDI YA MAPEPO WAHARIBIFU NA MAUAJI (05/8/2015)

Ee Mungu ninamfunga shetani mwaribifu na muuaji naanzisha mapambano dhidi ya uharibifu waliotumwa na shetani kuharibu mali zangu, Baba, imeandikwa katika Yer 51:25 “mimi ninapingana nawe ewe mlima mharibifu, mlima unaoharibu dunia nzima! Nasema mimi mwenyezi Mungu. Nitanyoosha mkono wangu dhidi yako, nitakuangusha kutoka mwambani juu ya kukufanya kuwa mlima uliochomwa moto” Baba niepushe na njia za Yule muovu anayenisumbua na ukamfunge shetani daima kwa jina la Yesu Kristo, Amina.

 

14. SALA YA KUJIKINGA NA MAOVU (06/8/2015)

Ee Yesu mwema ninaomba unikinge na maadui wowote wanaonizunguka, wateketeze na nguvu zao zote ambazo ninaziweka chini ya Ekarist Takatifu / chini ya msalaba wa Yesu, Amina.

 

15. SALA YA KUMFUNGA SHETANI (07/8/2015)

Ninamfunga mwovu anayenisumbua katika maisha yangu na ukoo wangu, ninamfunga na mamlaka yake yote, ufahamu wake wa kichawi naufunga na ninauweka chini ya msalaba Mtakatifu wa Yesu Kristo na vitu vyote vya kichawi visirudi tena na mwisho wakagombane wenyewe kwa wenyewe na kuomba msamaha katika jina la Yesu, Amina.

 

16. SALA YA UPONYAJI KATIKA JAMBO KUBWA

Wewe Mungu hukichukii kitu chochote ulichoumba bali wakipenda na kukistawisha, na kusihi uje hima kunisaidia katika jambo hili, Ee Bwana wewe ni pekee msaada wangu na kimbilio langu, wewe unajua namna unavyolishughulikia tatizo langu hili (taja tatizo) kama ni ugonjwa / msiba unaokusumbua. Ee Mungu Mwenyezi pokea maombi niliyokutolea ili kwa neema zako tuweze kuyapata kweli, Amina.

 

17. SALA YA KUJIKABIDHI KWA YESU

Ee Yesu naomba uwe pamoja nami katika hatari zote za Roho na mwili na ninajikabidhi Yesu mikononi mwako, lakini daima tuna matumaini makubwa katika wema na huruma yako takatifu, Amina.

Sala hii ya kujikabidhi kwa Yesu ilisisitizwa kusali mara kwa mara na hasa utakapokuwa unatoka nyumbani, hivyo kama familia sala hii tumekuwa tukisali kila siku yaweza kuwa zaidi ya mara moja, kadri Mungu alivyotubariki siku hiyo Amina.

 

18. SALA YA KUMFUKUZA SHETANI, JINI KAHABA

(Anayechukua watoto duniani) (15/10/2015)

Wewe jini kahaba kwa uwezo wa Mungu Mwenyezi ninakuamuru na kuvunjavunja silaha zako zote unazotumia kubeba watoto hapo duniani, ninaziharibu silaha hizo zote, ninakufunga wewe na mawakala wako wote, ninaamuru, mizimu, wachawi, rusifeli, mapepo, majini kuwaachia watoto wote, mabinti na nafsi za watu mlizozichukua ninawaamuru katika jina la Yesu muwarudishe ulimwenguni Amina.

 

19. SALA YA KUOMBEA NDUGU, JAMAA NA MARAFIKI WALIOTEKWA NA SHETANI

Baba Mungu Mwenyezi, ukawakomboe watu wako waliotekwa na shetani katika jina la Yesu Kristo, maana hao ni watu wako Mungu. Ninakuambia wewe shetani hauna mamlaka ya kuwashika watu wa Mungu, waachilie katika jina la Yesu Kristu na ninawakabidhi watoto wako Yesu mikono mwako, Amina.

 

20. SALA ZA KUVUNJA MAPEPO, MAJINI, VINYAMKELA NA KIKARAGOSI VINAVYOCHUKUWA VITU HAPA DUNIANI KAMA KUCHA, NYWELE, VIDOLE NA NYOTA YA MTU.

Baba ninavunja vunja nguvu za hawa viumbe ambao wanasoma nyota za watu wa Mungu, Baba ukawatume Malaika wako wa vita ili kuwateketeza hawa viumbe, Baba Mungu Mwenyezi ninaziharibu nguvu za hawa viumbe wanaochukua kucha, nyota, nywele, vidole, ulimi na ukateketeze miungu yao na hasa katika hiki kipindi kinachoendelea mpaka sasa, ninavunja ngome zao zote zilizoko Magharibi, Kaskazini, Mashariki na Kusini na kuziteketeza ngome hizo kwa moto wa Roho Mtakatifu, kwa jina la Yesu Kristo wa nazareti Amina.

 

Hizi ni baadhi ya sala chache alizoweza kuandika mtoto Grace ikiwa ni sehemu ya sala alizofundishwa na Mt. Michael Malaika Mkuu, na hasa alisisitiza wakristo wajenge tabia ya kabariki vitu wanapovinunua maana amegundua ujanja wa shetani, na kwa kubariki vitu vyetu tutakuwa tumefaulu kuvunja hila za shetani.

 

Japo sala hizi ni fupi Sali kwa imani sala utakayoichagua kila siku na kila mara.  Na Mungu atakujibu.

 

N.B Tutafurahi kupokea ushuhuda wako kupitia sala hizi.

 

©Imeandaliwa na:

Mtumishi: Julius Mmbaga

0766500747.

 

 

 


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

FAHAMU JINSI YA KUOMBA SALA YA VITA

MALAIKA MKUU MT. MICHAEL UTULINDE KATIKA VITA

SALA KWA AJILI YA KUFUNGULIWA KUTOKA KATIKA NGUVU ZA GIZA

CHANGAMOTO YA NDOTO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO

IBADA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

JINSI YA KUSALI ROSARI TAKATIFU YA BIKRA MARIA